Zari aeleza alivyoachana na Diamond

Muktasari:

Zari akwepa kuzungumzia iwapo Diamond atatuma watu wa kumwombea msamaha.


Dar es Salaam. Zari Hassan maarufu Zari The Boss Lady amesema hafikirii na hatarajii kurudiana na mzazi mwenzake Naseeb Abdul 'Diamond'.

Zari aliyezaa watoto wawili na Diamond ambaye ni msanii maarufu wa muziki ndani na nje ya nchi amesema hayo jana Februari 23,2018 alipohojiwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).

"Nilikaa muda mrefu nikafikiria vitu vingi ndipo nikasema unajua nini, nahitaji kufikia mwisho wa hili," amesema Zari alipoulizwa swali na mtangazaji Mariam Omary kuhusu ujumbe aliouweka katika akaunti yake ya kijamii ya Instagram akielezea kuachana na mzazi mwenzake.

Alipoulizwa ulikaa na kutafakari ukaona ufikie hili, Zari alijibu, "Tulikuwa tunajaribu kuona tuna-move kutoka  scandal (kashfa) ya kuwa amepata mtoto na tunaweza kusonga mbele."

"Lakini vitu kama hivi leo unasikia hivi leo unaona vile sijui kukumbatiana na ma X kwenye public, vitu vya kunidhalilisha, kunifanya nisiheshimike na watoto wangu, nimeachana naye kabisa," amesema.

Alipoulizwa iwapo Diamond alimpigia simu kumuomba msamaha baada ya picha hizo kusambaa, Zari amesema hakufanya hivyo na hakuona haja ya kumpigia simu kumuuliza.

Kuhusu Diamond kama atakwenda kumwomba msamaha atakubali Zari amesema, "Si alishakuja kipindi  fulani alipozaa na huyo dada fulani (Hamisa Mabeto) sioni kama itawezekana."

Alipoulizwa iwapo Diamond atatuma watu wa kumwombea msamaha; Zari amesema hawezi kulizungumzia hilo kwa kujibu 'no comment'.

Zari alipoulizwa iwapo hilo la kuachana ni kutafuta kiki amejibu, "Yaani tumeachana kabisa, it's done. Sijui kama amekubali, tangu video zile zimetoka na X wake nimem-block wiki tatu hatuongei ndipo nika-post."