Nyasi za Tanzania zinavyoinufaisha Australia

Muktasari:

Kirenga amesema hayo wakati akizungumzia namna Tanzania ilivyo fursa nyingi ambazo zimeachwa bila kuendelezwa au kushughulikiwa na wananchi ili kuwezesha Taifa kuendelea.

Dar es Salaam. Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Mpango wa Kuendeleza Kilimo Ukanda wa Kusini mwa Tanzania (Saggot), Geoffrey Kirenga amesema kama kuna jambo linaloumiza ni Australia kutumia nyasi kutoka Tanzania kwa ajili ya malisho na kisha kurejesha maziwa na nyama kutuuzia hapa nchini.

Kirenga amesema hayo wakati akizungumzia namna Tanzania ilivyo fursa nyingi ambazo zimeachwa bila kuendelezwa au kushughulikiwa na wananchi ili kuwezesha Taifa kuendelea.

“Lakini cha kushangaza, Australia wanatumia nyasi za Tanzania kulisha ng’ombe wao halafu wanakuja kutuuzia nyama na maziwa,” amesema.

Ameongeza kuwa,“vilevile tuna tatizo la kuhifadhi chakula, mahindi yanayozalishwa nchini kwa mwaka ni kati ya tani milioni 6 hadi 7, lakini yanayohifadhiwa kwa njia za kisasa ni kati ya tani milioni moja hadi mbili yaliyobaki yanahifadhiwa kwa njia za kienyeji, yanaishia kuharibika. Ipo haja kwa Serikali ikatengeneza maghala katika maeneo ya uzalishaji.”  

Kirenga akasema katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, Tanzania ina fursa nyingi za kilimo lakini tatizo ni  kukosa uthubutu na taarifa za uhakika.

 Naibu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Saggot, Jennifer Baarn amesema wanaangalia matatizo yanayorudisha nyuma sekta ya kilimo na namna ya kuyatatua ili kuhakikisha mnyororo wa kuongeza thamani ya mazao unaleta tija kwa wakulima, hasa wadogo.