Nyumba ‘yajaa’ matundu ya risasi Vikindu

Nyumba ambayo polisi waliivamia kwa ajili ya kuwakamata watu wanaotuhumiwa ni majambazi ambapo dirishani inaonyesha matobo ya risasi, iliyopo eneo la Vikindu, wilayani Mkuranga, Mkoa wa Pwani. Picha na Said Khamis

Muktasari:

Matundu hayo yamekutwa wakati Jeshi la Polisi likisema mapambano makali bado yanaendelea.

Dar es Salaam. Nyumba walimokuwa wanaishi majambazi eneo la Vikindu, Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, imekutwa ikiwa na matundu ya risasi zaidi ya 50 hali iliyoashiria mpambano ulikuwa mkali.

Matundu hayo yamekutwa wakati Jeshi la Polisi likisema mapambano makali bado yanaendelea.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro amesema jana kuwa mapambano makali yanaendelea.

Hata hivyo,  Sirro hakutaka kufafanua kwa undani, wala kutaja idadi ya waliouawa katika tukio hilo.

Kamanda Sirro alisema wamepeleka polisi zaidi ya 80 katika eneo hilo kuimarisha usalama.

“Operesheni inaendelea na sisi tunahakikisha silaha zote zilizoibwa zinarudishwa na ifikapo Jumanne ripoti kamili itatolewa,” amesema.