Pacha walioungana wapata maajabu matokeo kidato cha sita

Watoto mapacha walioungana, Maria na Consolata ambao walikuwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Udzungwa kwa sasa wanajipanga kuendelea na masomo ya chuo kikuu. Mapacha hao wamefanya vizuri katika  matokeo ya kidato cha sita yaliyotoka juzi. Picha ya Maktaba.

Muktasari:

Wamesema wamepokea vizuri matokeo na hawajui wampe nini Mungu

Dar es Salaam. Pacha walioungana, Maria na Consolata Mwakikuti wamefanya maajabu mengine baada ya kufaulu mitihani yao ya kidato cha sita kwa kupata matokeo sawa ya Daraja la Pili.

Pacha hao wenye ndoto za kuwa walimu walifanana kwenye matokeo ya darasa la saba walipohitimu katika Shule ya Msingi Ikonda wilayani Makete kwa kupata alama sawa.

Hata hivyo, wakiwa Shule ya Sekondari ya Maria Konsolata wilayani Kilolo, Iringa walitofautiana kwenye ufaulu wa kila somo kwenye matokeo ya kidato cha nne.

Na safari hii watu wengi walikuwa wakisubiri kusikia matokeo ya pacha hao ambao miezi kadhaa iliyopita walikuwa gumzo nje na ndani ya nchi baada ya kuhitimu kidato cha sita.

Wakizungumzia matokeo ya kidato cha sita yaliyotangazwa juzi na Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), Maria na Consolata walimweleza mwandishi wetu kuwa wameyapokea kwa furaha kwa kuwa yanawapa nafasi ya kuendelea na masomo ya chuo kikuu.

Wamesema wameyapokea vizuri na hawajui wampe nini Mungu.

Pacha hao wamesema wanatamani kupata nafasi ya kuendelea na masomo katika Chuo Kikuu cha Ruaha (Rucu) ili iwe rahisi kwao kuendelea kulelewa na walezi wao, Shirika la Masista la Maria Consolata.

Pacha hao wamehitimu kidato cha sita katika Shule ya Sekondari Udzungwa na mwalimu mkuu wa shule hiyo, Edward Fue amesema kufaulu kwao kunaiongezea heshima nyingine ya kipekee shule hiyo.

“Japo shule yetu ina mwanafunzi mmoja aliyepata sifuri, kwa kweli matokeo ya watoto hawa yameisuuza mioyo yetu. Hakika tuna furaha isiyo kifani kwa sababu kila mmoja hapa shuleni alikuwa akiwaombea kwa dini yake ili wafaulu. Maria na Consolata wameonyesha mfano mzuri,” amesema.

Mwalimu Fue alisema shule hiyo ilijitahidi kuwaandalia mazingira mazuri ili kuhakikisha ndoto yao kielimu inatimia, jambo ambalo limefanikiwa.

Katika matokeo hayo, Udzungwa ilikuwa na wahitimu 76 na watatu wamepata daraja la kwanza, 36 daraja la pili wakiwamo Maria na Consolata, 31 daraja la tatu, wanne daraja la nne na mmoja amepata ziro.

Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Iringa, Ritta Kabati amesema kufaulu kwa mabinti hao ni fundisho kwa watoto wa kike na watu wote wenye ulemavu nchini.

“Nawafahamu Maria na Consolata, ni wasichana wanaojituma, hivyo kufaulu ilikuwa haki yao. Hili liwe funzo kwa watu wengine wenye ulemavu kwamba, wanaweza kufanya maajabu wakiamua,” amesema Kabati.