Papa ataka kanisa lifunge kuombea DRC, Sudan Kusini

Muktasari:

Nchi zote mbili zinakabiliwa na usalama mdogo na mgogoro wa  binadamu katika miaka michache iliyopita. Baba Mtakatifu ameomba kuingilia kati kiroho akiwaomba waumini waaminifu kufunga na kuomba kwa ajili ya amani ya nchi hizo Februari 23

 Papa Francis ametangaza Ijumaa ya Februari 23 kuwa siku ya kufunga na sala kwa ajili ya kuziombea Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Congo (DRC) na Sudan Kusini zinazokumbwa na migogoro ya kisiasa.

Nchi zote mbili zinakabiliwa na usalama mdogo na mgogoro wa binadamu katika miaka michache iliyopita. Baba Mtakatifu ameomba kuingilia kati kiroho akiwaomba waumini waaminifu kufunga na kuomba kwa ajili ya amani ya nchi hizo Februari 23.

Pia, mkakati huo una lengo la kutafuta amani ulimwenguni. Papa amewaalika waumini wengine waaminifu wasio Wakatoliki kushiriki katika kutafuta amani ya nchi mbili hizo na duniani kote.

Wito wake ulijibiwa na Mkuu wa Kanisa la Anglikana la Kimataifa, Justin Welby, ambaye aliwaagiza watu kufuata wito wa Papa. Pia, Welby alielezea uzoefu wa kile alichokiona katika safari za awali DRC na Sudan Kusini.

"Katika ziara yangu kwenye nchi hizo mbili miaka ya hivi karibuni, ilikuwa haiwezekani kuelezea kiwango kikubwa cha uharibifu. Migogoro hii inasababisha kupotea uhai wa watu wengi. Idadi kubwa ya watu imelazimika kukimbia nyumba zao, ambako kunasababisha familia na jamii kuvunjika.

"Kuna idadi mpya ya zaidi ya watu milioni moja waliotawanyika ndani ya nchi. Njaa inasababisha mateso makubwa na hatari. Katika Sudan Kusini, watu milioni sita wanakabiliwa na njaa. Vurugu za unyanyasaji na udhalilishaji wa kijinsia hufanywa kwa kiwango kibaya sana katika nchi zote mbili.

"Wakati wa ziara yangu ya mwisho, nilimsikiliza kiongozi wa kisiasa akiniambia kuhusu mateso na mauaji ya watu wake. Nilitembelea kambi ya wakimbizi nchini Uganda iliyojaa watoto wa Sudan Kusini ambao familia zao zilikimbia nyumba zao ili kuepuka mauti," ilisema taarifa rasmi.

Alitoa pia masuala ambayo waamini wanaweza kuomba wakati wa kufunga:

 

• Viongozi wa Sudan Kusini na DRC wageuze mioyo yao kutoka vita hadi amani - na kutafuta ufumbuzi wa amani kwa matatizo ya kisiasa.

• Kwa wakimbizi wote kutoka nchi hizi.

• Kwa msamaha, uponyaji na mahusiano mapya.

• Kwa makanisa ya mitaa kufanya mengi ya kuwaangalia watu ambao wanateseka, na kuleta amani.

Hali nchini DRC kwa kiasi kikubwa inakwamishwa na hatua ya kuendelea kubaki madarakani kwa Rais Joseph Kabila ambaye muhula wake ulimalizika mwishoni mwa mwaka 2016. Kushindwa kuandaa uchaguzi kulimaanisha yeye kuendelea kubaki ofisini.

Maandamano ya dhidi ya Kabila yaliyoandaliwa na vikundi vya kiraia likiwemo kanisa yamevunjwa kikatili. Uchaguzi, hata hivyo, umepangwa kufanyika baadaye mwaka huu. Kabila, walio karibu naye wanasema, hatagombea na ameahidi kuteua mrithi mwezi Julai mwaka huu.