Pengo awataka maaskofu kuhubiri umoja wa Taifa

Muktasari:

  • Ametoa kauli hiyo leo Sumbawanga mkoani Rukwa

Dar es Salaam. Mwadhama Kadinali, Polycarp Pengo amewataka maaskofu kuhubiri umoja kwa waumini wao.

Pengo amesisitiza hilo leo Jumapili Juni 24, 2018 katika misa ya kumuweka wakfu Askofu wa Jimbo Katoliki Sumbawanga, Beatus Urassa inayofanyika katika Kanisa Kuu la Epifania mjini humo na kurushwa moja kwa moja na Redio Tumaini.

“Katika kuliongoza Tanzania ni muhimu sisi maaskofu tusisitize juu ya umoja wa waamini waliokombolewa kwa damu moja ya Kristu. Kwa mazingira ya Tanzania, wewe na mimi na maaskofu wote tusisitize umoja wa Watanzania na Tanzania,” amesema Pengo.

“Tusikubali  kuziruhusu damu mbalimbali zinazotufanya kuwa wenye kabila hili au lile zikatawala na kuvunja umoja  wa Taifa letu. Tuombeane katika kazi hii. Tutunze umoja wa waumini na wa Taifa letu.”

Amesisitiza, “Wewe umezaliwa mkoani Kilimanjaro ni mchaga unayetoka Rombo. Katika utandawazi wa Tanzania siku hizi ni muhimu kuzingatia yafuatayo, unayo damu ya kichaga ndani ya mwili wako, nakuomba wala usikatae na usijaribu kuificha damu hii.”

“Hakuna sababu wala uhalali kwako wa kujaribu kuficha ukweli huu. Neno moja lazima ulikumbuke ni kuwa wewe na mimi na kundi lote hatujakombolewa kwa damu ya kichaga wala ya kifipa na kinyakyusa, sote tumekombolewa kwa damu ya Kristo.”

Askofu Urassa anachukua nafasi ya Mhashamu Damian Kyaruzi ambaye amestaafu.