Polisi, TCRA ‘watangaza kiama’ cha wanaotumia mitandao vibaya

Muktasari:

Msako unaendelea kuwatafuta wanaotumia mitandao vibaya au kinyume cha sheria

Dar es Salaam. Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na  Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA) wameanza msako ili kubaini wanaofanya makosa ya mtandao.

Akizungumza na MCL Digital leo, Kamanda wa Kanda hiyo, Lazaro Mambosasa alisema polisi kwa kushirikiana na TCRA watahakikisha wote wanaofanya makosa ya mtandao wanakamatwa.

“Nitatoa taarifa zaidi lakini jua operesheni ndiyo imeanza na haitakuwa na mwisho. Tutahakikisha wote wanaofanya makosa tunawakamata mpaka waishe,” alisema Mambosasa.

Kauli hiyo ya Mambosasa imekuja baada ya mwandishi wa Mwananchi kumuuliza iwapo kukamatwa kwa baadhi ya wasanii na watu maarufu nchini ni operesheni maalumu au ni kutokana na malalamiko.

Akifafanua alisema kukamatwa kwao kunatokana na msako maalumu na kwamba mpaka kufikia jana watu nane walikuwa wamekamatwa.

“Inawezekana mpaka sasa idadi ya waliokamatwa imeongezeka lakini sijachukua taarifa, ninafahamu kuhusu watu nane tu ambao tunawashikilia kwa mahojiano zaidi,” alisema.