Polisi wamtaka Sheikh Ponda ajisalimishe ndani ya siku tatu

Muktasari:

Kamanda Mambosasa amesema kukimbia hakutamsaidia Sheikh Ponda.

Dar es Salaam. Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, imemtaka Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Issa Ponda kujisalimisha ndani ya siku tatu kuanzia leo Alhamisi kwa kosa la kutoa lugha ya uchochezi.

Kamanda wa kanda hiyo, Lazaro Mambosasa amesema  ni vyema Sheikh Ponda akajisalimisha kabla hajatafutwa.

Mambosasa amesema jana Jumatano Sheikh Ponda alitumia lugha ya uchochezi alipozungumza na waandishi wa habari na kutoa kejeli kwa Serikali.

Amesema kukimbia kwake hakutasaidia chochote ni vyema ajitokeze kwa ajili ya kuhojiwa kuhusu suala hilo.

“Sheikh Ponda alikuwa anajua kwamba anafanya kosa kwa sababu aliwaambia waandishi waje saa nne yeye akawapigia baadhi waje kabla ya saa nne,’’ amesema.

Kamanda Mambosasa amesema baada ya askari kufika eneo ambalo Sheikh Ponda alikutana na waandishi wa habari,  waliwachukua waandishi na wafuasi wake kwa mahojiano.

Amesema baada mahojiano na Polisi kujiridhisha waliwaachia huru.