Polisi wachunguza kupigwa mwanahabari

Muktasari:

Imesema imefungua jalada la uchunguzi

Dar es Salaam. Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema polisi imeanza uchunguzi wa tukio la kupigwa kwa mwandishi wa habari wa Wapo Redio, Sillas Mbise.

Mbise anadaiwa kushambuliwa na polisi juzi Agosti 8, 2018 wakati wa mchezo kati ya Simba na Asante Kotoko ya Ghana.

Video za tukio hilo zimesambaa katika mitandao ya kijamii, zikimuonyesha Mbise akishushiwa kipigo na polisi.

Akizungumza leo Ijumaa Agosti 10, 2018 Mambosasa amesema polisi wameanza uchunguzi wa tukio hilo kwa kufungua jalada la uchunguzi wa picha hizo za video.

Amesema hiyo inakwenda sambamba na kumtaka mtendewa wa kosa hilo la kupigwa kutoa taarifa kituo cha polisi ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.

Amesema mtu yeyote anatakiwa kutoa malalamiko yake pale anapoona ametendewa vitendo ambavyo ni kinyume cha sheria.