Polisi wadhibiti dawa za kulevya JNIA, lakini…

Muktasari:

  • Mbushi amesema hata hivyo inawezekana wahalifu hao wamebuni mbinu mpya.

Dar es Salaam. Kamanda wa Polisi wa Viwanja vya Ndege, Matanga Mbushi amesema wamedhibiti mianya ya upitishaji wa dawa za kulevya katika Viwanja vya Ndege vya Mwalimu Nyerere (JNIA).

Akizungumza na Mwananchi leo Mei 27, Mbushi amesema katika kipindi cha Februari hadi Mei mwaka huu miezi mitatu hawajakamata mhalifu yeyote wa dawa za kulevya.

“Hii ni kutokana na kudhibiti mianya ya usafirishaji wa dawa hizo, tofauti na zamani,” amesema.

Mbushi amesema kutokamatwa wahalifu hao JNIA huenda pia ni kiashiria kuwa wamebuni njia nyingine ambazo hazijatambulika.

“Wafanyabiashara hao haramu inawezekana wamebuni mbinu mpya nyingine ambazo hatuzifahamu hivyo tumejipanga na kuendelea kuwadhibiti ili uwanja wa JNIA usitumike kama uchochoro wa kupitisha dawa za kulevya,” amesema Mbushi.

Ametoa wito kwa wananchi washirikiane na vyombo husika wanapoona kuna mtu anajihusisha na dawa za kulevya kwa kuwa vita hii ni ya watu wote inatakiwa ushirikiano wa hali ya juu.