Polisi wafanya doria mtandaoni

Muktasari:

  • Usambazaji wa taarifa za uongo mitandaoni ni changamoto sugu

Dar es Salaam. Licha ya kuwepo kwa sheria ya makosa ya mtandao, usambazaji wa taarifa za uongo mitandaoni umeendelea kuwa changamoto sugu.

Kutokana na hali hiyo, kitengo cha polisi cha makosa ya mtandao kinaendelea kufanya doria mitandaoni ili kuwabaini wahusika hao na wengine wa makosa ya mtandao.

Joshua Mwangasa, naibu mkuu wa kitengo hicho amesema hayo leo Ijumaa wakati wa uzinduzi wa awamu ya pili ya kampeni ya matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii. 

Amesema kuna kesi nyingi za watu kusambaza taarifa za uongo kwa makusudi na wengine bila kufahamu kuwa ni kosa kisheria.

"Hatuingilii mawasiliano binafsi, sisi tunachunguza yale ambayo yanawafikia wanajamii, huko tunagundua wapo wanaofanya kwa makusudi na wengine hawafahamu kama ni kosa kisheria, lakini kutojua sheria si utetezi," amesema Mwangasa.

Mmiliki wa Blogu ya Fikra Pevu, Maxence Melo amesema waendeshaji wa blogu wanakabiliwa na changamoto ya watumiaji kutojua sheria.

"Wengi hawajui hizo sheria zilizopo, utakuta mtu anaandika maoni hadi unajiuliza alifikiria nini kuandika hiki, hii inatupa wakati mgumu kuanza kupitia maoni ya kila mmoja. Kama huna muda ndiyo unakuta vitu visivyofaa vinasomeka," amesema Melo.