Polisi waua watatu wanaodaiwa majambazi Mwanza

Muktasari:

Watuhumiwa hao wameuawa katika majibizano ya risasi na polisi

Dar es Salaam. Polisi mkoani Mwanza wamewaua watuhumiwa watatu wa ujambazi baada ya majibizano ya risasi kati yao na askari wa jeshi la polisi huku wengine watatu wakikimbia.

Polisi pia wamefanikiwa kukamata bunduki aina ya ‘shotgun’ na magazine mbili zikiwa na risasi mbili na maganda mawili.

Kaimu kamishna wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi amewataja waliouwawa leo (Ijumaa) kuwa ni Benedict Tobias, Mabula Segeja na Charles Thomas huku wenzao watatu wakikimbia.

“Askari walipowabaini majimbazi hao katika eneo ambalo walipanga kukutana waliawataka kujisalimisha lakini majambazi hao walikaidi na kuanza kurusha risasi ambayo ili mjeruhi mwenzao ndipo askari nao wakaanza kujibu ,”amesema Msangi.

Amesema miili ya watuhumiwa hao wa ujambazi imehifadhiwa katika hospitali ya rufaa Bugando kwa ajili ya uchunguzi na utambuzi.

Kamanda huyo amesema  msako wa kuwatafuta waliokimbia bado unaendelea.