JPM amrudishia hadhi ya ubalozi Profesa Mahalu

Muktasari:

Mtu yeyote ambaye amewahi kutumikia katika cheo cha balozi, huendelea kupewa heshima ya balozi katika maisha yake yote hata baada ya kustaafu katika nafasi ya utumishi wa umma.

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amemrudishia Profesa Costa Mahalu hadhi ya ubalozi kuanzia leo Machi 17, 2018.

Profesa Mahalu alisimamishwa kazi na kuvuliwa hadhi ya ubalozi mwaka 2007 baada ya kufunguliwa mashtaka ya Jinai na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hata hivyo, mwaka 2012, Mahakama ilitoa hukumu kwamba, Profesa Mahalu hakuwa na hatia.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika MasharikiProfesa Adolf Mkenda  inabainisha kuwa kutokana na taratibu za utumishi, mtu yeyote ambaye amewahi kutumikia katika cheo cha balozi, huendelea kupewa heshima ya balozi katika maisha yake yote hata baada ya kustaafu katika nafasi ya utumishi wa umma.  

“Kutokana na uamuzi wa rais, Profesa Mahalu sasa ataendelea kuwa na heshima ya kuitwa balozi,” ilinukuu sehemu ya taarifa hiyo.