RC aagiza polisi kukamatwa aliyeshinda zabuni

Muktasari:

  • Agizo hilo amelitoa leo Machi 8  baada ya meya wa manispaa hiyo, Chifu Karumuna kulalamika kwenye kikao cha bodi ya barabara kuwa mkandarasi huyo amewaingiza hasara kwa kuwa aliingia kwenye ushindani wa zabuni, akashinda  na baadaye akakataa kusaini mkataba hali iliyosababisha mchakato uanze upya.


Bukoba. Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Meja Jenerali mstaafu, Salum Kijuu amemuagiza kamanda wa polisi mkoani humo kumsaka na kumkamata mkandarasi wa kampuni ya Mecco aliyeshinda zabuni ya Sh6 bilioni za ujenzi wa barabara za lami katika Manispaa ya Bukoba na baadaye kugoma kujitokeza kusaini mkataba.

Agizo hilo amelitoa leo Machi 8  baada ya meya wa manispaa hiyo, Chifu Karumuna kulalamika kwenye kikao cha bodi ya barabara kuwa mkandarasi huyo amewaingiza hasara kwa kuwa aliingia kwenye ushindani wa zabuni, akashinda  na baadaye akakataa kusaini mkataba hali iliyosababisha mchakato uanze upya.

Amekieleza kikao hicho kuwa kampuni ya Mecco ilishinda tenda kwa kuwa na sifa ya ziada ya kujenga kiwanja cha ndege cha Bukoba, ambapo aliomba msaada wa Serikali kwa kuwa fedha hizo zimetolewa na Benki ya Dunia na kuwa wananchi wanacheleweshwa kupata barabara imara.

Akifunga kikao hicho, mkuu wa mkoa ameagiza mkandarasi huyo asakwe, akamatwe na kupelekwa ofisini kwake akiwa na pingu akisisitiza kuwa hawezi kuruhusu ubabaishaji unaokwamisha maendeleo ya wananchi.