Rais Magufuli aivunja KDA

Muktasari:

KDA ni Mamlaka ya Usimamizi wa Mji Mdogo wa Kigamboni ambayo hivi sasa shughuli zake zitafanyika kwenye manispaa

Rais John Magufuli ameivunja Mamlaka ya Usimamizi wa Mji Mdogo wa Kigamboni (KDA) na  sasa shughuli zake zinahamishiwa katika Manispaa ya Kigamboni.

Akizungumza leo Jumatano,Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amesema ametumwa na Rais Magufuli kutangaza uamuzi huo.

"Kumekuwa na mgongano katika usimamizi wa ardhi kati ya KDA na Manispaa ya Kigamboni, Rais ameliona hilo na kuamua kuivunja mamlaka hiyo,"amesema.

Lukuvi amesema jukumu la KDA lilikuwa kusimamia upangaji wa mji wa Kigamboni wakati hilo pia ni jukumu la manispaa hiyo.

Lukuvi ametoa miezi sita kwa watendaji wa KDA kukamilisha makabidhiano ya nyaraka na wao kuripoti kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigamboni.

Mapema Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Hashim Mgandilwa amesema mgongano wa usimamizi wa ardhi Kigamboni ulisababisha migogoro mingi ya ardhi.

Amesema pia manispaa hiyo ina upungufu wa maofisa mipango miji.

Amesema manispaa ina maofisa mipango miji watatu badala ya saba wanaohitajika.