Rais Magufuli awanyanyua CAG, Katibu Mkuu kujibu suala la Sh1.5 trilioni

Muktasari:

Rais Magufuli amefanya hivyo baada ya kueleza kuwa ameona watu wanapostiposti upotevu wa fedha hizo ambazo yeye amesoma ripoti ya CAG na hakuziona


Dar es Salaam.Rais Joh Magufuli amewanyanyua Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali(CAG),  Profesa Mussa Assad na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Dotto James kueleza kama kuna upotevu wa Sh 1.5 trilioni kama inavyodaiwa.

Rais Magufuli aliwataka watendaji hao waeleze hilo leo Ijumaa Aprili 20, Ikulu wakati akizungumza baada ya kumaliza kuwaapisha majaji wapya kumi aliowateua hivi karibuni.

“Kuna watu wanaposti posti vitu kwenye mitandao kwamba kuna upotevu wa shilingi trilioni 1.5 mimi nimefuatilia hilo sijaona upotevu huo. Niliposikia taarifa hizo nikampigia CAG mbona kwenye ripoti yako uliyoniletea hapa Ikulu hukuonyesha hilo eneo la upotevu hilo akaniambia hakuna... maana angeniambia tu siku ile ile hata kama ni waziri ningemtimua,” amesema.

Baada ya kueleza hivyo, Rais Magufuli alianza kuwahoji watendaji hao akitaka wathibitishe kama kweli upotevu huo umetokea.

“Bahati nzuri CAG yuko hapa... embu tuthibitishie kama fedha hizo kweli zimepotea,” amesema Rais Magufuli kabla CAG kusimama na kujibu; “mheshimiwa hapana... hakuna upotevu uliokuwepo.” Baada ya CAG kutoa majibu hayo Rais Magufuli akamhoji Katibu Mkuu Wizara Fedha na Mipango asimame kujibu swali hilo hilo.

“ Hakuna upotevu huo mheshimiwa Rais...Hazina tuko salama,” alisema Dotto. Rais Magufuli aliendelea kusisitiza kutokuwepo kwa opotevu huo huku akionyesha kusikitisha namna watu wanavyotumia uhuru wa mitandao kutuma yale wanayoyapenda.

“Kwa vile hii mitandao hatukotro sisi basi watu wanapostiposti vitu wavitakavyo hata kama siyo vya kweli,” amesema.