Rais wa Misri kutua nchini wiki ijayo

Dar es Salaam. Rais wa Misri, Abdel Fattah Al Sis anatarajiwa kufanya ziara ya siku mbili nchini ikiwa ni ziara yake ya kwanza katika eneo la Afrika Mashariki tangu aingie madarakani mwaka 2014.

Ingawa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Aziz Mlima hakuwa tayari kutaja tarehe ya kuwasili kwake mbali ya kusisitiza kuwa kiongozi huyo atawasili wiki ijayo lakini duru za habari zinasema huenda akatua nchini Agosti 14.

Ujio wa kiongozi huyo inafuatia mwaliko kutoka kwa mwenyeji wake, Rais John Magufuli ambaye alikutana naye kwa mara ya kwanza wakati alipohudhuria mkutano wa Umoja wa Afrika, Addis Ababa Ethiopia.

Tanzania na Misri zimekuwa na uhusiano wa karibu kwa muda mrefu uhusiano uliofufuliwa na viongozi waasisi wa mataifa hayo, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Gamal Abdel Nasser.

Viongozi hao walikuwa mstari wa mbele katika harakati za kupigania uhuru wa Afrika na kukabiliwa na utawala wa kikoloni na kibaguzi. Pia, walikuwa miongoni mwa waasisi waliopigania jitihada za kuliunganisha bara la Afrika.

Kulingana na Katibu Mkuu, Dk Aziz, Rais Al Sis anatarajiwa kuongozana na ujumbe wa watu kadhaa na pindi atakapowasili atapokelewa na mwenyeji wake, Rais Magufuli na kisha wote watakuwa na mazungumzo ya faragha kabla ya baadaye kuzungumza na wananchi.

Nchi hizo mbili zimekuwa na ushirikiano katika maeneo yanayogusa jamii, uchumi, siasa na yale yanayohusu ulinzi na usalama.

Misri inatajwa kuwa ni nchi ya pili kwa kuwa na uchumi mkubwa barani Afrika huku uwekezaji wake kwa Tanzania ukifikia Dola za Marekani 887.02 milioni. Kulingana na takwimu kutoka Kituo cha Uwekezaji Nchini (TIC) Misri imewekeza katika miradi nane na hivyo kusaidia kutoa ajira kwa watu wanaokadiriwa kufikia 953.