Rais wa Zimbabwe avunja baraza la mawaziri

Muktasari:


  • Mnangagwa aliyeapishwa Ijumaa kuchukua nafasi ya Robert Mugabe aliyejiuzulu chini ya shinikizo la jeshi na wananchi amemrejesha Patrick Chinamasa kwenye wizara ya fedha na Simbarashe Mumbengegwi katika wizara ya mambo ya nje.
  • Rais ...amevunja baraza la mawaziri, na kwa sasa yuko katika mchakato wa kuunda timu mpya ya mawaziri.

 Rais Emmerson Mnangagwa amevunja baraza la mawaziri na ameteua jipya, wakiwemo washirika wake wawili kusimamia kwa umadhubuti Wizara ya Fedha na Mambo ya Nje.

Mnangagwa aliyeapishwa Ijumaa kuchukua nafasi ya Robert Mugabe aliyejiuzulu chini ya shinikizo la jeshi na wananchi amemrejesha Patrick Chinamasa kwenye wizara ya fedha na Simbarashe Mumbengegwi katika wizara ya mambo ya nje.

Hatua hiyo imefikiwa wakati Wazimbabwe wakisubiri kwa shauku kubwa orodha mpya ya baraza la mawaziri wakitaka kuona kama atateua sura mpya au ataendelea na waliokuwa watiifu kwa mtangulizi wake.

Gumzo jingine ni ikiwa Mnangagwa atajumuisha baadhi ya wapinzani kusaidia kujenga na kuimarisha uchumi ulioharibiwa.

Chinamasa na Mumbengegwi walikuwa wanasimamia wizara hizo kabla ya kushushwa katika mabadiliko yaliyofanywa na Mugabe mwezi uliopita. Katika mabadiliko hayo ambayo yaliwasukuma nje washirika wa Mnangagwa ndiyo yaliyochangia kuhitimisha utawala wa miaka 37 wa Mugabe wiki iliyopita.

Taarifa ya Katibu wa Baraza la Mawaziri Misheck Sibanda Jumatatu ilithibitisha kuteuliwa kwa Chinamasa na Mumbengegwi.

"Rais ...amevunja baraza la mawaziri, na kwa sasa yuko katika mchakato wa kuunda timu mpya ya mawaziri,” alisema Sibanda. Aliongeza kwamba Chinamasa na Mumbengegwi tayari wameshateuliwa kuwa kaimu mawaziri ili "zisivurugike huduma muhimu kwenye wizara husika".