Safari ya Hawa wa Diamond India yaotea mbawa Airport

Muktasari:

Msanii Hawa Said aliyekuwa aondoke leo kwenda nchini India kwa matibabu amejikuta akishindwa kufanya hivyo baada ya kutokuwa na kibali cha daktari kupanda ndege.


Dar es Salaam. Msanii Hawa Said maarufu Hawa wa Diamond, amejikuta akirudishwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam (JNIA) baada ya kutotimiza vibali vya kusafiri vya kimatibabu kwenda India.

Akizungumza na MCL Digital baada ya kukwama leo Oktoba 13, 2018  meneja wa Diamond Platinumz ambao ndiyo wamechukua jukumu la kugharamia matibabu hayo, Babu Tale amesema hali hiyo imewakuta wakiwa tayari wameingia ndani ya uwanja wa ndege na kuanza kukaguliwa nyaraka zao mbalimbali.

Babu Tale amesema nyaraka iliyowakwamisha kusafiri ni kibali cha daktari kuelezea hali ya mgonjwa  ili wahudumu ndani ya ndege wajue namna watakavyomhudumia.

"Kuna mgonjwa anaweza akawa katika hali ya kuzimia, kutapika anatakiwa ahudumiwe tofauti, hivyo Hawa imeshindikana kwa kuwa hakuna hizo nyaraka inayoonyesha hivyo kutoka kwa daktari na wametwambia turudi itakapokamilika," amesema.

Hawa, Babu Tale na mama yake, Ndagina Hassan ilikuwa waondoke leo  saa 10:45 na ndege ya Shirika la Emirates.

Hawa na mama yake, Ndagina, walifika uwanjani hapo tangu saa 7:00 mchana huku Babu Tale akiwasili saa 9:00 alasiri.

MCL Digital iliyokuwa imepiga kambi wakati wote uwanjani hapo, ilifanikiwa kuzungumza na mama wa Hawa ambaye ameelezea furaha yake ya mwanaye kupata msaada wa matibabu.

Naye Hawa amewaomba Watanzania kumuombea dua katika matibabu hayo.

Awali, Babu Tale amesema walitarajia kuwa nchini humo kwa wiki mbili na huenda Hawa akapandikizwa ini kama madaktari watashauri hivyo. Mwisho