Sauti ya Lissu yamliza Mkuu wa KKKT

Muktasari:

Askofu Shoo amesema kupona kwa Lissu ni jibu la Mungu na onyo kwa wote waliohusika.

Moshi. Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Frederick Shoo amesimulia alivyobubujikwa machozi baada ya kusikia sauti ya Rais wa Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS), Tundu Lissu.

Dk Shoo ambaye pia ni Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini, amesema hayo baada ya Jumatano Oktoba 18,2017 Lissu kutoa salamu akiwashukuru Watanzania kupitia video iliyosambaa kwenye mitandao ya kijamii.

Lissu anaendelea na matibabu katika Hospitali ya Nairobi nchini Kenya baada ya kushambuliwa na kujeruhiwa kwa risasi Septemba 7,2017 mjini Dodoma.

Sauti ya Lissu katika video hiyo ilikuwa ni ya kwanza kusikika tangu apelekwe jijini Nairobi Septemba 7.  Alisikika akiwashukuru madaktari wa Nairobi na Hospitali ya Rufaa ya Dodoma kwa kuokoa maisha yake.

Pia, amewashukuru viongozi wa dini na wananchi kwa kumuombea, na taasisi za kitaaluma  ndani na nje ya nchi ikiwemo TLS ambazo zilionyesha mshikamano mkubwa.

Akizungumza na Mwananchi, Askofu Shoo amesema alijikuta akitokwa machozi aliposikia sauti ya Lissu, akisema kupona kwake ni onyo kwa wale waliohusika.

 “Ninazidi kumshukuru Mungu kwa jinsi alivyomuokoa na anavyozidi kumpa uponyaji. Kupona kwa Lissu ni jibu la Mungu na onyo kwa wale wote waliohusika. Mungu amesema hapana,” amesema.

Askofu Shoo amesema, “Mwenye masikio na asikie. Uhai wa mwanadamu ni kitu cha kuheshimu. Tusijaribiwe kujichukulia madaraka ya kuondoa uhai wa mtu hata kama uwezo tunao kwa maana Mungu hataki na wala hataacha kumwadhibu yeye aondoaye uhai wa ndugu yake kwa hiana.”