Sauti feki ya Makonda ‘yawaliza’ Wachina

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Simon Sirro

Muktasari:

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Simon Sirro alisema jana ofisini kwake kuwa Oktoba Mosi, mwaka huu mfanyakazi wa Kampuni ya Group Six ambaye  ni raia wa China, Marco Li (24) alipigiwa simu na mtu aliyejitambulisha kuwa ni Makonda.

Dar es Salaam. Raia wa China wametapeliwa fedha taslimu Sh22.8 milioni wakidai kuwa sauti waliyoisikia kwenye simu ya kiganjani iliyotumiwa na tapeli ilifanana na ya  Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Simon Sirro alisema jana ofisini kwake kuwa Oktoba Mosi, mwaka huu mfanyakazi wa Kampuni ya Group Six ambaye  ni raia wa China, Marco Li (24) alipigiwa simu na mtu aliyejitambulisha kuwa ni Makonda.

Sirro alisema tapeli huyo alimtaka raia huyo atoe Dola 3,500 za Marekani kwa ajili ya msaada wa kumsomesha mwanafunzi aliyechaguliwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Manilla kilichopo nchini Ufilipino.

“Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Jensen Hung (39) alikubali ombi la mkuu wa mkoa huyo feki na kumtuma msaidizi wake, Marco Li aende ofisini kwake kwa ajili ya kujiridhisha,” alisema Sirro.