Scorpion afunguliwa mashtaka upya

Muktasari:

Amefunguliwa mashtaka mengine yanayofanana na ya awali ya unyang’anyanyi wa kutumia silaha.

Dar es Salaam. Mahakama ya Wilaya ya Ilala, imemfungulia  mashtaka mapya Salum Njwete (Scorpion).

Amefunguliwa mashtaka mengine yanayofanana na ya awali ya unyang’anyanyi wa kutumia silaha.

Hata hivyo Njwete amekana shtaka na kurudishwa rumande,huku Hakimu Flora Haule anayesimamia kesi hiyo akizuia dhamana.

Awali Mahakama hiyo ilimfutia mashtaka yanayomkabili Scorpion baada ya upande wa mashtaka kuomba shtaka hilo liondolewe mahakamani kwa sababu hawana nia ya kuendelea na kesi hiyo na Kutokana na maombi hayo,  Hakimu Adelf Sachore alikubaliana na ombi hilo kwa kuzingatia kifungu namba 91 kifungu kidogo cha kwanza cha sheria ambacho kinampa Mamlaka Mkurugenzi Wa Mashtaka nchini (DPP) kuondoa shtaka mahakamani muda wowote ili mradi kama kesi hiyo haijatolewa hukumu.

Lakini kifungu hicho kinampa Mamlaka DPP kumshtaki upya mshtakiwa huyo kama ana nia ya kuendesha shtaka hilo.

Njwete anakabiliwa na shtaka la unyang'anyi wa kutumia silaha na kumjeruhi Saidi Mrisho.