Sembe yapanda bei Zanzibar

Muktasari:

Baadhi ya wakazi, walisema kupanda kwa kasi kwa bidhaa hiyo kunayafanya maisha yao kuanza kuwa magumu kiasi cha wengi wao kushindia urojo na ubwabwa.

Zanzibar. Bei ya unga wa sembe imeendelea kupanda kisiwani Unguja mpaka kufikia Sh2,200 kwa kilo moja, kutoka kiasi cha Sh900 Desemba mwaka jana.

Baadhi ya wakazi, walisema kupanda kwa kasi kwa bidhaa hiyo kunayafanya maisha yao kuanza kuwa magumu kiasi cha wengi wao kushindia urojo na ubwabwa.

Mpaka jana mchana katika mtaa wa Amani bei ya sembe ilikuwa Sh1,900, Magazeti Sh1,700, Al-Tabibu Sh1,800, Magomeni Sh1,800, Msumbiji Sh1,900 na Mji Mkongwe Sh2,200.

Mfanyabishara katika soko la Mwanakwerekwe, Ustaadhi Ally Rashid alisema walianza kununua viroba vya unga kwa bei ya juu tangu Desemba, hivyo walilazimika kuuza kwa Sh900 kwa kilo.

“Kwa jumla nanunua kiroba cha kilo 25 kwa Sh40,000 siwezi kuuza bei ya hasara. “Mahindi yamepanda bei kutokana na ukame ndicho tunachoambiwa, ” alisema.

Muuzaji katika soko hilo, Juma Ramadhani (69) alisema bei hiyo inatokana na viwanda vinavyozalisha unga kuuza kwa bei ya juu bidhaa hiyo kwa sasa, lakini bei zimekuwa zikipanda taratibu japokuwa mwaka huu hali imebadilika.

“Nakumbuka Rais wa Awamu ya Pili, Mzee (Ali Hassan) Mwinyi alipoondoka ilikuwa Sh30 alipoingia (Benjamin) Mkapa ikafikia Sh300 alipomkabidhi (Jakaya) Kikwete ikafikia Sh700 sasa hivi tumefika huku,” alisema.