Serikali kufungua akaunti kusaidia waathirika ajali ya MV Nyerere

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenista Mhagama

Muktasari:

  • Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenista Mhagama amesema uongozi wa Mkoa wa Mwanza utafungua akaunti maalum kwa ajili ya kukusanya fedha zitakazosaidia walioathirika na ajali ya kuzama kwa Kivuko cha MV Nyerere

Dar es Salaam. Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenista Mhagama amesema uongozi wa Mkoa wa Mwanza utafungua akaunti maalum kwa ajili ya kukusanya fedha zitakazosaidia walioathirika na ajali ya kuzama kwa Kivuko cha MV Nyerere.

Mhagama ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Septemba 22, 2018 wakati kampuni ya mawasiliano ya simu ya Vodacom ikikabidhi msaada wa Sh10milioni kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe katika kisiwa cha Ukara, wilayani Ukerewe Mkoa wa Mwanza.

Amesema akaunti hiyo inafunguliwa kutokana na sheria ya maafa inayoelekeza kuwa yanapotokea maafa Mkoa husika unapaswa kufungua akaunti itakayotumika kukusanya fedha kusaidia waathirika.

Ametoa rai kwa Watanzania na kampuni mbalimbali kuchangia fedha kusaidia waathirika wa ajali na kwamba fedha hizo zitatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

“Fedha zitakazopatikana zitasaidia waliopoteza ndugu na manusura wa ajali,” amesema.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella amewatoa wasiwasi wananchi watakaochangangia akisema fedha zitakazopatikana zitatumika kwa kile kilichokusudiwa.

“Tupo kwenye mchakato wa kufungua akaunti leo hii lakini Mwanza hakuwezi kutokea kama ya Kagera, “ amesema Mongella akikumbushia fedha za kusaidia waliokumbwa na tetemeko la ardhi mkoani Kagera zilivyotafunwa kinyemela.

“Sisi hatutaruhusu na niwahakikishie watu wote wenye nia njema ya kusaidia walioathirika watuamini. Katika hili hatutakuwa na mzaha na yeyote yule atakayecheza na ajali na kuigeuza fursa.”