Serikali yaingia mgogoro na wafanyakazi

File Photo

Muktasari:

Wafanyakazi hao hawajalipwa mishahara inayokadiriwa kufikia takriban Sh700 milioni kuanzia Februari.

Mwanza. Wafanyakazi zaidi ya 100 wa Kampuni ya Huduma za Meli (MSCL), ambao hawajalipwa mishahara kwa takriban miezi minane mfululizo wanatarajiwa kulifikisha suala hilo mbele ya Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA).

Wafanyakazi hao hawajalipwa mishahara inayokadiriwa kufikia takriban Sh700 milioni kuanzia Februari.

Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Meli na Bandari Tanzania, Jonathan Msoma amethibitisha kuwapo kusudio hilo. Amesema ofisi yake ipo katika hatua za mwisho za maandalizi, ikiwamo kuwasiliana na wanasheria ili malalamiko yao yapatiwe ufumbuzi wa kisheria.

Kaimu Meneja wa MSCL, Beatus Rugarabamu amesema wafanyakazi hao hawajalipwa mishahara kutokana na uchakavu wa meli na ofisi yake imeomba msaada kutoka serikalini.