Serikali yajipanga kutumia Sh 32.4 trilioni mwaka wa fedha 2018/19

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimpongeza Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango kwa kuwasilisha bungeni Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/2019, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Serikali inatarajia kukopa Sh8.90 trilioni kutoka soko la ndani na nje 

Dodoma. Akizungumzia sura ya bajeti ya mwaka 2018/19 Mpango amesema kuwa  kwa kuzingatia shabaha na sera za bajeti kwa mwaka 2018/19, inaonyesha kuwa jumla ya Sh32.48 trilioni zinatarajiwa  kukusanywa na kutumika katika kipindi hicho.

Hayo yamesemwa leo Juni 14  na Waziri wa Fedha na Mipango Phillip Mpango bungeni mjini Dodoma wakati akiwasilisha bajeti kuu ya serikali kwa 2018/19.

Soma bajeti nzima hapa: http://bit.ly/BAJETIMW

Amesema jumla ya mapato ya ndani (ikijumuisha mapato ya Halmashauri) yanatarajiwa kuwa Sh20.89trilioni sawa na asilimia 64.3 ya bajeti yote.

Amefafanua kati ya mapato hayo, Serikali inalenga kukusanya mapato ya kodi ya jumla ya Sh18.0trilioni sawa na asilimia 13.6 ya pato la taifa.

Ameeleza  mapato yasiyo ya kodi yanakadiriwa kuwa Sh 2.16trilioi na mapato kutoka vyanzo vya Halmashauri Sh735.6 bilioni.

“Washirika wa maendeleo wanatarajiwa kuchangia Sh2.68 trilioni ambayo ni asilimia 8.2 ya bajeti yote,” amesema

Amefafanua  misaada na mikopo hiyo inajumuisha misaada na mikopo nafuu ya miradi ya maendeleo Sh2.0 trilioni, mifuko ya pamoja ya kisekta Sh125.9bilioni na misaada na mikopo nafuu ya kibajeti Sh545.8 bilioni.

Mpango amesema   Serikali inatarajia kukopa Sh8.90 trilioni kutoka soko la ndani na nje kwa masharti ya kibiashara, mikopo ya ndani inatarajiwa kuwa Sh5.79 trilioni ambapo Sh4.6trilioni ni kwa ajili ya kulipa dhamana za serikali zinazoiva na Sh1.19trilioni  ni mikopo mipya kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo.