Serikali yampokonya Sumaye shamba lake Dar

Muktasari:

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Hapi amesema kuwa Serikali imefikia uamuzi huo baada ya Sumaye kushindwa kuliendeleza kama notisi ya siku 90 ilivyoeleza.

Dar es Salaam. Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye amepokonywa na Serikali shamba lake lenye ukubwa wa hekta 33 kwa kile kilichoelezwa kushindwa kuliendeleza.

 

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Hapi amesema kuwa Serikali imefikia uamuzi huo baada ya Sumaye kushindwa kuliendeleza kama notisi ya siku 90 ilivyoeleza.

 

“Oktoba 28, mwaka huu. Rais John Magufuli alibatilisha hati ya kumiliki ardhi ya shamba namba 3074 lililopo Mabwepande. Shamba hili lilikuwa na hati namba 53086. Jina la mmiliki lililoandikwa katika hati ni Frankline Sumaye,” amesema Hapi.

 

Sumaye ambaye alikuwa ni mmoja wa wasemaji tegemeo katika mikutano ya kampeni ya Uchaguzi Mkuu uliopita ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), anamiliki mashamba makubwa yaliyoko Morogoro na Mabwepande Dar es Salaam.

 

Baada ya Rais Magufuli kubatilisha hati hiyo, Hapi amesema kuanzia sasa ni marufuku kwa Sumaye kujihusisha na shamba hilo.

 

Kwa sababu hati yake imeshabatilishwa na akibainika kufanya chochote vyombo vya dola vitachukua nafasi yake.

 

“Vyombo vya ulinzi na usalama watakuwapo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba shamba hili halitafanyiwa shughuli zozote, isipokuwa baada ya taratibu za manispaa zitakapofanyika,” amesisitiza Hapi.

 

Amesema amemwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Kinondoni, Aron Kagurumjuli kupima viwanja vya shamba hilo na kwamba wananchi waliokuwa na mgogoro wa shamba hilo wafikiriwe.

 

Februari 5 mwaka huu, akiwa Morogoro, Rais John Magufuli aliwataka watu wote waliotelekeza mashamba kuyaendeleza, la sivyo atawanyang’anya na kuwapa wananchi.

 

Alipotafutwa kwa simu, Sumaye amesema hana taarifa hizo na kwamba yupo nje ya Dar es Salaam na badala yake alimwomba mwandishi amweleza aliyesimamia mchakato huo.

 

Baada ya kuelezwa Sumaye amesema: “Unataka nieleze nini wakati umeniambia Rais (Magufuli) amebatilisha. Ila niseme tu nikirudi Dar es Salaam nitalifuatilia na kuchukua hatua zinazostahiki.”