Serikali yataka nidhamu bendera ya Taifa

Muktasari:

Chibogoyo alisema jana kuwa taasisi hiyo inataka kurudisha maadili na uzalendo kwa wananchi kuheshimu alama za Taifa.

Dar es Salaam. Mpigachapa Mkuu wa Serikali, Cassian Chibogoyo ameonya matumizi yasiyo sahihi ya bendera ya Taifa na wimbo akitaka watendaji kusimamia maadili vinginevyo watachukuliwa hatua za kinidhamu.

Chibogoyo alisema jana kuwa taasisi hiyo inataka kurudisha maadili na uzalendo kwa wananchi kuheshimu alama za Taifa.

Alisema watendaji wanaopeperusha bendera zilizochakaa na kupauka wanafanya makosa kwani kunaidhalilisha Serikali kwa kuwa mpya zinapatikana bila ya urasimu.

“Baadhi ya watendaji wamekuwa wakiacha bendera zinapeperuka hadi usiku wakati sheria inataka zishushwe saa 12.00,” alisema.

Alifafanua kuwa wananchi wanatakiwa kusimama kwa utulivu wakati bendera ya Taifa inapopandishwa na kushushwa.

“Tofauti na zamani, siku hizi bendera ya Taifa inapopandishwa watu wanapita na kupiga kelele kama vile hakuna jambo linalotokea,” alisema.

Kuhusu wimbo wa Taifa, Chibogoyo alisema haupaswi kuimbwa kwenye vilabu vya pombe bali kwenye mikusanyiko rasmi ya kiserikali.

“Huu siyo wimbo wa kuimbwa ovyo, lazima turudishe maadili yetu Watanzania,” alisema.

Mpigachapa huyo alisema viongozi, watendaji na wananchi wanatakiwa kujifunza na kuufahamu wimbo huo na kuonyesha hisia za kizalendo kwa nchi.