Sh225 mil zahudumiwa wanafunzi hewa

Muktasari:

Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkulu alisema kamati maalumu aliyounda imebaini uwapo wa wanafunzi hewa 29,000, ambao wamekuwa wakiisababishia hasara Serikali kila mwezi.

Kahama. Wanafunzi hewa waliobainika wilayani Kahama, wameisababishia hasara Serikali ya Sh225 milioni kwa kipindi cha miezi minane kuanzia Januari hadi Agosti.

Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkulu alisema kamati maalumu aliyounda imebaini uwapo wa wanafunzi hewa 29,000, ambao wamekuwa wakiisababishia hasara Serikali kila mwezi.

“Serikali ya Awamu ya Tano tangu iingie madarakani imekuwa ikituma fedha kila shule kwenye mpango wa elimu bure, lakini maofisa elimu, waratibu kata, walimu wakuu wa shule za msingi na sekondari wamebuni mbinu za kula fedha hizo kwa kuweka wanafunzi hewa kwenye shule zao,” alisema Nkulu.

Alitoa siku tatu kwa kila halmashauri kuwasilisha takwimu sahihi za wanafunzi ambazo zitalingana na idadi aliyonayo iliyopatikana baada ya kamati ya uchunguzi.