Mwigulu aongoza uchomaji moto shamba la bangi ekari sita

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba akiteketeza bangi katika kijiji cha Engalaoni Wilaya ya  Arumeru mkoani Arusha leo Februari 7, 2018. Picha na Moses Mashalla.

 


Muktasari:

Mwigulu asema operesheni hiyo ni endelevu na inafanyika nchi nzima.


Arumeru. Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba ameongoza operesheni ya kuteketeza ekari sita za bangi zilizokuwa zimelimwa katikati ya msitu uliopo kijiji cha Engalaoni wilayani Arumeru mkoani Arusha.

Uteketezaji huo umefanyika leo Februari 7, 2018 ambapo Mwigulu, Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Charles Mkumbo na baadhi ya askari wamelazimika kutembea kwa miguu umbali wa kilomita 2 kwenda katika msitu huo, huku wamiliki wa mashamba wakitokomea kusikojulikana.

Bangi hizo zilivunwa kutoka shambani, kurundikwa sehemu moja na kisha kuchomwa moto.

Mwigulu amesema Serikali itaendelea na operesheni hiyo nchi nzima na haitasita kuwakamata wahusika wote na kutaifisha magari yanayotumika kusafirisha bangi.

Amewataka polisi kuongeza juhudi kupambana na wanaotengeneza dawa za kulevya viwandani.

Kwa upande wake Mkumbo amesema ekari sita za mashamba ya bangi zimeteketezwa na kusisitiza kwamba operesheni hiyo ni endelevu katika mkoa wa Arusha na wilaya zake.

Amesema kwa sasa wanaolima bangi wamebuni mbinu ya kulima katikati ya misitu ili kukwepa kukamatwa.

“Wananchi wanapaswa kubadilika kwa kulima mazao yenye tija badala ya bangi. Polisi kama walinzi wa usalama hatutakubali kuona vijana wanaathirika kwa matumizi ya dawa za kulevya,” amesema.

“Walidhani kulima bangi katikati ya misitu hatutawabaini. Polisi tuna mbinu nyingi na hatutakubali kuona vijana wetu wanaharibikiwa kwa sababu ya bangi.”