Jeshi la polisi lamshikilia Ponda kwa mahojiano

Muktasari:

Kuhusu uwezekano wa dhamana, Profesa Safari amesema hilo litategemea polisi watakavyoamua huku akisema tuhuma zinazomkabili zina dhamana na ni kauli za kawaida ambazo amerejea matukio yaliyotokea.

Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, linamshikilia Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda akituhumiwa kutoa lugha za kichochezi.

Inadaiwa juzi Jumatano, Sheikh Ponda akizungumza na waandishi wa habari alizungumzia masuala mbalimbali ya kisiasa na kutoa taarifa ya kile alichozungumza na Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu alipokwenda kumtembelea hospitali ya Nairobi nchini Kenya.

Kutokana na kile alichokizungumza, jana Alhamisi, Kamanda wa Polisi Kanda ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa alitoa saa 72 kwa Sheikh Ponda kujisalimisha, wito alioutekeleza leo Ijumaa asubuhi akiwa ameambatana na mawakili wanne wakiongozwa na Profesa Abdallah Safari.

Profesa Safari akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kutoka ndani kwa kupisha swala ya Ijumaa amesema: “Sheikh Ponda wamemshikilia kwa muda, kwani sisi wanasheria wake wote ni Waislamu, tumewaomba twende kuswali tutarejea baadaye,”

“Unajua mimi nimekuwa hapo toka saa 3 asubuhi, tumefanya mahojiano na mdomo, wameweka clip ya kile alichozungumza juzi, wamemwonyesha na ‘Press release’ baadaye wakasema wanaanza mahojiano ya maandishi saa 6.15 mchana sie tukasema twende msikitini kwanza na tukasema tutarudi kama saa 8 au saa 9,” ameongeza:

Kuhusu uwezekano wa dhamana, Profesa Safari amesema hilo litategemea polisi watakavyoamua huku akisema tuhuma zinazomkabili zina dhamana na ni kauli za kawaida ambazo amerejea matukio yaliyotokea.

“Alizungumzia hali ya jumla ya kisiasa, akazungumzia jinsi alivyokwenda kumwona Tundu Lissu…lakini kama wataamua kumshikilia na kutaka kumpeleka mahakamani basi nitaongoza jopo la wanasheria mimi mwenyewe nyani mzee kwenda kumtetea rafiki na mwanaharakati mwenzangu,” amesema Profesa Safari ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Chadema-Bara