Shilole aeleza waliomshauri kufunga ndoa kimyakimya

Muktasari:

Amesema sherehe kubwa itafanyika hivi karibuni.

Dar es Salaam. Mwanamuziki Zuwena Mohammed maarufu Shilole amesema aliamua kufunga ndoa kimyakimya baada ya kushauriwa na viongozi wa dini.

Pia, ameeleza alivyopata upinzani kutoka kwa dada yake ambaye hakutaka aolewe na mwanamume aliyemchagua.

Ndoa ya Shilole ilizua gumzo baada ya kufanyika katika hali ya kushtukiza licha ya kuwa aliahidi angefunga kwa uwazi na kufuatiwa na sherehe kubwa.

Shilole akizungumza na mwandishi wa mtandao wa Millard Ayo, amesema aliamua kufunga ndoa kimyakimya na mpenzi wake Uchebe baada ya kuambiwa ndoa haitangazwi kwa sababu inaweza kukaribisha uadui.

“Niliambiwa si kila mtu anapenda kusikia jambo jema kama hilo, wengine wanaweza kukufanyia husuda usifanikishe kwa hiyo nikaamua kuwasikiliza lakini haimaanishi kuwa sitafanya sherehe,” amesema.

Akizungumzia familia yake kumzuia kufunga ndoa amesema, “Unajua hayo ni mambo ya kifamilia, nina watoto wawili halafu ananichagulia mwanamume wa kuolewa naye?”

Shilole amesema anatarajia kufanya sherehe kati ya Desemba 25 na Desemba 27,2017.

“Sherehe ya kukata na shoka nitaitangaza siku mbili hizi. Itakuwa ya aina yake kwa kuwa watu watakula, kunywa na vingine kubeba. Itakuwa ya kihistoria,” amesema.