Shirika latoa nguo za ndani 750 kwa waathirika Kagera
Muktasari:
Msaada huo ulikabidhiwa jana kwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera Meja Jenerali Mstaafu,Salum Kijuu.
Bukoba. Shirika la Tanganyika Christian Refugees Service (TCRS)limetoa vifaa vya Sh 82 milioni zikiwamo nguo za ndani 750 kwa waathirika wa tetemeko la ardhi mkoani Kagera.
Msaada huo ulikabidhiwa leo kwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera Meja Jenerali Mstaafu,Salum Kijuu.
Kadhalika shirika hilo limekabidhi sufuria,mablanketi na ndoo za maji kwa ajili ya kusambazwa kwa waathirika wa tetemeko hilo.
Oscar Rutenge, Meneja wa shirika hilo kutoka tawi la Shinyanga alisema lengo la msaada huo ni kuwasitiri wanawake.
“Katika janga hili walioathirika wengi ni wanawake hizo nguo za ndani lengo lake ni kutaka kuwasitiri ndiyo maana tumetoa hata kanga na taulo sisi tumekabidhi kwenye kamati ya maafa tuna imani vitafika.” alifafanua Rutenge
Misaada mingine iliyotolewa na shirika hilo ni ndoo za maji na miche ya sabuni vyote vikiwa na thamani ya 82 milioni ambapo shirika hilo hutoa misaada mbalimbali wakati wa maafa yakiwemo yaliyotokea eneo la Mwakata Mkoani Shinyanga.