Siku tatu za Makonda zilivyotikisa Dar es Salaam

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda

Muktasari:

  • Aliingia studio za Clouds TV Ijumaa usiku akiwa na askari waliokuwa na silaha za moto, akajadiliwa katika mitandao ya kijamii kutokana na kitendo hicho, Jumapili akawa sehemu ya mahubiri ndani ya Kanisa la Uzima na Ufufuo, lakini jana Rais John Magufuli akamhakikishia kibarua chake, jambo lililoongeza kasi ya mjadala.
  • “Makonda Amtega Rais Magufuli”, “Makonda Katika Moto kwa Kuvamia Clouds Usiku”, Makonda, Gwajima Waanza Vita Upya”, na “Makonda ‘Ateka’ Clouds Media” ni baadhi ya vichwa vya habari vya magazeti ya jana kuonyesha kitendo cha mkuu huyo wa mkoa kilivyotikisa nchi.

Dar es Salaam. Kwa siku tatu mfululizo, mjadala mkubwa umekuwa ni jina la mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda.

Aliingia studio za Clouds TV Ijumaa usiku akiwa na askari waliokuwa na silaha za moto, akajadiliwa katika mitandao ya kijamii kutokana na kitendo hicho, Jumapili akawa sehemu ya mahubiri ndani ya Kanisa la Uzima na Ufufuo, lakini jana Rais John Magufuli akamhakikishia kibarua chake, jambo lililoongeza kasi ya mjadala.

“Makonda Amtega Rais Magufuli”, “Makonda Katika Moto kwa Kuvamia Clouds Usiku”, Makonda, Gwajima Waanza Vita Upya”, na “Makonda ‘Ateka’ Clouds Media” ni baadhi ya vichwa vya habari vya magazeti ya jana kuonyesha kitendo cha mkuu huyo wa mkoa kilivyotikisa nchi.

Habari hizo zote zinazungumzia kitendo cha Makonda kuingia studio za Clouds TV inayomilikiwa na Clouds Media Ijumaa usiku, akiwa na askari waliovalia sare na kiraia na ambao walishika silaha za moto na kukariri wadau wakitaka Rais amchukulie hatua.

Na jana asubuhi wadau wa habari, Waziri Nape Nnauye, mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari (Moat), Jukwaa la Wahariri (TEF), wahariri, wasanii na vyombo vingine vya habari vilikuwa vikitoa pole kwa uongozi wa Clouds na kulaani kitendo hicho cha Makonda.

Huku wananchi wakiendelea kupaza sauti kutaka atengue uteuzi wa mkuu huyo, Rais Magufuli alitumia ufunguzi wa mradi wa ujenzi wa barabara za juu za kupishana magari katika makutano ya Barabara ya Sam Nujoma na Morogoro kueleza ya moyoni kuhusu mkuu huyo wa mkoa wa Dar es Salaam.

Rais alizungumzia taarifa zinazoendelea kujadiliwa mitandaoni kuwa hazina tija na kumtaka “Makonda aendelee kuchapa kazi”.

Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na mjadala mkubwa mtandaoni kuhusu Makonda na utata wa elimu yake, utajiri wa ghafla na tukio la Ijumaa usiku. Ilikuwa ni takriban saa tatu baada ya mkurugenzi wa vipindi na uendeshaji wa Clouds Media, Ruge Mutahaba kuzungumza kuhusu tukio hilo katika kipindi cha televisheni cha 360, ambacho Rais Magufuli ameshapiga simu mara tatu kueleza jinsi anavyokifuatilia.

Ruge alikuwa akithibitisha habari zilizoenea mitandaoni tangu Jumamosi kuwa Makonda alifika studio za Clouds TV Ijumaa usiku, akiwa ameambatana na askari wenye silaha za moto na kuchukua kwa nguvu sehemu ya kipindi cha Shilawadu kilichokuwa kimezuiwa kurushwa kutokana na kutokidhi matakwa ya kitaaluma.

Shilawadu ni kifupisho cha Shirikisho la Wambea Duniani na ni kipindi ambacho kinazungumzia tuhuma za watu mbalimbali maarufu na katika mahojiano ya 360, Ruge alisema alihisi habari ambayo aliizuia isitoke hadi itakapokidhi vigezo vya kitaaluma, ilikuwa ina uhusiano na Makonda baada ya kuambiwa na mmoja wa watangazaji wa Shilawadu kuwa inamuhusu mwanamke ambaye anadai amezaa na Askofu Josephat Gwajima, mpinzani mkubwa wa mkuu huyo wa mkoa.

Taarifa kuhusu Makonda kuhusika katika sakata hilo zilipamba moto Jumapili asubuhi na zikafuatiwa na video zinazomuonyesha mkuu huyo wa mkoa akiingia ofisi hizo akiwa na askari wenye silaha.

Kusambaa kwa video hizo kuliibua mjadala mkubwa kutokana na wengi kuhoji sababu za Rais Magufuli kutochukua hatua haraka kama alivyofanya kwa watumishi wengine wa umma, akiwemo Charles Kitwanga aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani baada ya kuingia bungeni akiwa amelewa.

Kutokana na maswali mbalimbali kuibuka, huku Clouds ikitakiwa ieleze ukweli, Ruge alilazimika kueleza kilichotokea, akitumia kipindi cha televisheni ya Clouds TV cha 360 kinachorushwa kila siku asubuhi.

“Paul (Makonda) ni rafiki yetu, lakini ametukosea, huwezi kuja ofisini kwetu ukiwa na mabunduki tena usiku,” alisema Ruge ambaye vituo vyake vya redio na televisheni vimekuwa vikirusha moja kwa moja shughuli za Makonda.

“Sijutii urafiki wetu na mkuu wa mkoa, bali nalaumu vitendo vyake na anapokosea lazima aambiwe ukweli kuwa kakosea. Makonda ni rafiki yetu, lakini mimi urafiki na bunduki siutaki kabisa. Urafiki wa wali na maharage freshi.”

Ruge, ambaye usoni alionekana kuwa asiyetaka masihara, alisema hakutaka kumtafuta Makonda baada ya tukio hilo kwa kuwa mkuu huyo wa mkoa ndiye aliyewakosea.

“Nataka nirudie kwamba urafiki unatengeneza mazingira ya kwamba, ok. Hii unataka kuifanya vizuri zaidi, kitengenezee mazingira mazuri zaidi. Tutakuruhusu ufanye, sio hapa atafanya hata kule kama ambavyo tunaruhusu watu wengine pia wafanye,” alisema Ruge.

“Mimi kwa kweli nampongeza upande mmoja; ni mtu ambaye kwa kweli amekuwa akitumia nafasi vizuri, kwa sababu sio kosa kusema kwamba mimi nina hiki, naomba niki-edit vizuri mnisaidie kukirusha, sio kosa. Kosa ni pale ambapo unapotaka kupanda watu kichwani.

“Kosa ni pale ambapo unapotumia nafasi yako kwa ubaya.”

Ruge alisema yeye anasimamia chombo kilicho na watu zaidi ya 200 na ambao ni vijana wadogo, kulinganisha na Makonda ambaye anasimamia watu milioni tano.

“Kwa bahati mbaya wale mia mbili wananitazama kama mtu ambaye ni mfano. Nisipowatetea wao, huyu atakuja leo. Akija kila siku kiongozi mwingine?” alihoji Ruge.

“Tubadilishe mtazamo wetu sasa maana viongozi wanashindana na wasanii kutafuta kiki kwenye mitandao ya kijamii. Viongozi wetu wanapenda kumzungumzia Mwenyezi Mungu, lakini hawajui kuwa dhambi za binadamu zinaumiza zaidi kuliko kumuudhi Mungu.”

Msimamo wa Magufuli

Hata hivyo, Rais John Magufuli alimtaka Makonda kuendelea kuchapa kazi na kwamba yeye hafanyii kazi maneno ya kwenye mitandao.

Magufuli, ambaye wakati mwingi wa hotuba yake alionekana akisoma, alionekana kuanza kutotegemea alichokiandaa alipoanza kuzungumzia suala la Makonda.

Alisema kuna baadhi ya watu wanaingilia majukumu yake wakati yeye ndiye mwenye uamuzi na kwamba hapangiwi kazi ya kufanya kwa sababu anajiamini.

“Tunaendekeza mambo ya udaku wakati hayatusaidii kupata chakula, kupunguza foleni Dar es Salaam, kupeleka watoto shule, kupata maji ya kunywa, kupata maendeleo. Tuzungumze uchumi na maendeleo ya wana-Dar es Salaam,” alisema Rais Magufuli.

“Mnahangaika kupost (kutuma) mara hili, mara lile, mpaka watu wengine wananiingilia nifanye mambo wanayotaka. Ukinipangia ndiyo unapoteza. Mimi ni Rais ninayejiamini.”

Kwa wiki takriban tatu, kumekuwa na habari katika mitandao zikimuhusisha Makonda na mtu anayeitwa Daudi Bashite aliyesoma Shule ya Msingi Koromije na Sekondari ya Pamba na kumaliza kidato cha nne kwa kupata daraja la sifuri.

Mmoja kati ya watu wanaoongoza kushamirisha habari hizo ni Askofu Gwajima, ambaye amesema anamfahamu na anao ushahidi wa vyeti na watu waliosoma na Bashite na hivyo kumtaka Makonda athibitishe utambulisho wake, la sivyo ataweka bayana kila kitu.

Lakini Rais Magufuli, ambaye Serikali yake imekuwa ikifanya uhakiki wa wafanyakazi wa umma na elimu yao, alisema habari za mitandaoni hazina tija kwake na kuwataka wakazi wa Dar es Salaam kuchapa kazi kwa ajili ya maendeleo badala ya kupoteza muda kufuatilia udaku kwenye mitandao.

Alisema hawezi kupangiwa nini cha kufanya.

“Najua mwenyewe nani anatakiwa kuwa wapi, akae wapi, ni mimi ninayepanga. Ninajua wamenielewa,” alisema Rais.

“Kwa hiyo Makonda wewe chapa kazi. Nasema chapa kazi. Suala la kuandikwa kwenye mitandao sio tija kwangu. Hata mimi ninaandikwa kwenye mitandao, kwa hiyo nijiuzulu urais? Chapa kazi,” alisema Rais akimuangalia Makonda, ambaye alisimama na kuinamisha kichwa kuonyesha kukubali.

“Kwa hiyo niwaombe ndugu zangu Watanzania, tunapoteza muda mwingi kwa mambo yasiyo ya msingi. Tuwatumikie Watanzania. Watanzania wana shida nyingi za kufanya. Wanahitaji maji, wanahitaji barabara, wanahitaji elimu, wanafunzi wa chuo kikuu wanahitaji wapate mikopo, Ni mambo yote. wanahitaji afya nzuri. Hilo ndilo jukumu letu sisi viongozi.

“Kwa hiyo niwaombe Watanzania wenzangu wa vyama vyote, tusijisumbue na mambo yasiyo na msingi.”

Ruge asimulia

Kabla ya kutoa hotuba hiyo, Ruge alieleza mkasa wote ulivyokuwa tangu Alhamisi wakati Makonda alipoenda makao makuu ya Clouds na kuongea na watangazaji wa kipindi cha Shilawadu.

Ruge alisema siku hiyo walikuwa na kikao na watu wa TCRA na baada ya hapo alitoka nje ambako alimkuta Makonda akiwa pamoja na vijana wanaofanya kipindi cha Shilawadu na alipowauliza kuwa ni kwema alijibiwa kuwa walikuwa katika mazungumzo ya kawaida tu.

“Nikiwa kwenye gari nikijiandaa kutoka, kijana mmoja wa Shilawadu alinifuata na kuniambia kuna mahojiano amefanya na mtu anaedai amezaa na Gwajima nikamuuliza kwa hiyo,” alisema Ruge.

Alisema kijana huyo alimwambia kuwa wameshindwa kumpata Gwajima na hivyo akawaambia wasirushe hicho kipindi hadi wampate askofu huyo.

Na kwa kuweka msisitizo, Ruge alimwambia meneja wa vipindi anayeitwa Kerry kuwa kama Askofu Gwajima hajapatikana, kipindi hicho kisirushwe na baadaye kumpigia simu ofisa rasilimali watu kumweleza suala hilo.

Pia, Ruge aliwaambia waandaaji wa kipindi hicho wamueleze hata Makonda kuwa hawangeweza kukirusha kutokana na upande wa pili kutopatikana.

“Tena nikamwambia Kerry kwa masihara kuwa ikiwezekana ayapoteze kabisa hayo ‘material’ kwa sababu hata Shilawadu wenyewe walikuwa wanavutana juu ya habari hiyo,” alisema Ruge.

Ruge aliendelea kuwa siku hiyo hiyo saa 10:00 jioni alipigiwa simu na Askofu Gwajima akimueleza kuwepo kwa habari inayomuhusu, lakini akamhakikishia kuwa habari hiyo haipo na haitaruka kwa sababu haijakidhi vigezo.

Mkurugenzi huyo alisema jambo la kushangaza majira ya saa 4:45 usiku Ijumaa alipokea simu kutoka kwa ofisa rasilimali watu akimueleza kuwa mkuu wa mkoa ameingia ofisini akiwa na askari sita wenye silaha.

Alisema baada ya simu hiyo ilifuatia simu ya mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo, Joseph Kusaga akimueleza kuwa analaumiwa na Makonda kuwa amezuia kipindi chake.

Mtangazaji mualikwa wa 360, Masoud Kipanya aliuliza kama Makonda huwa ana vipindi vyake Clouds, lakini Ruge alisema hakuna kitu kama hicho.

Alisema baadaye Kusaga alitaka wafanye mazungumzo na Makonda kuhusu suala hilo.

“Mimi nikamwambia siwezi kwenda kwa sababu hata mkuu wa mkoa hajaonyesha heshima kwa sababu anao uwezo wa kunipigia simu muda wowote. Kwa nini hajafanya hivyo mpaka avamie,” alisema Ruge.

Ruge alisema baadaye alimpigia simu Makonda na akamuuliza sababu za kwenda ofisi za Clouds na watu wenye bunduki, lakini Makonda akamjibu kuwa amefanya hivyo kwa sababu amezuia kipindi chake.

“Kwanza sio kipindi chako (Makonda). Mimi ndiye mkurugenzi wa vipindi, na hivi vipindi viko chini yangu,” alisema Ruge akikumbuka mazungumzo yake na Makonda kwenye simu.

Ruge alisema Makonda alimuelezea kuhusu kipindi kinachomuhusu mwanamke anayedai amezaa na Askofu Gwajima, lakini akamjibu kuwa upande wa pili haujapatikana na kumueleza umuhimu wa kusimamia weledi kwa kila mtu kupewa nafasi.

Alisema Clouds kama chombo cha habari wameumia kuona tukio hilo linafanywa na rafiki yao ambaye angeweza kuhoji kwa namna nzuri  lakini sasa amesababisha vijana wa Shilawadu kutokuwa sawa mpaka wamefikia hatua ya kuomba likizo ili watulize akili zao kwa kuwa tayari washaingiwa uoga.

“Tubadilishe mtazamo wetu sasa maana viongozi wanashindana na wasanii kutafuta kiki kwenye mitandao ya kijamii. Viongozi wetu wanapenda kumzungumzia Mwenyezi Mungu lakini hawajui kuwa dhambi za binadamu zinaumiza zaidi kuliko kumuudhi Mungu,” alisema Ruge.

Alisema video zinazosambaa katika mitandao ya kijamii likihusisha tukio lile ni za kweli, lakini hajui ni nani aliyezitoa kwa sababu pale kuna CCTV kamera na kila mfanyakazi anajua wapi zinafanyia kazi.

Pia alizungumzia habari zilizosambaa kuwa alishikiliwa na polisi Jumapili.

“Watu walisema eti niliwekwa ndani polisi lakini sio kweli nilienda tu kuripoti kwa ajili ya taarifa maana linapotokea jambo lolote linalohusu uvamizi wa silaha ni lazima maelezo yachukuliwe ili kuepusha upotoshaji,” alisema Ruge.

Pia, Ruge alisifu vyombo vya habari kwa kumuonyesha mshikamano, akisifu hata wapinzani wao wakubwa kwamba wamesikitishwa na tukio hilo na kuomba wadau wote wa habari kusimama pamoja katika hilo kuhoji haki na heshima ya vyombo vya habari.

Nape awatembelea

Katika tukio jingine, hata kabla ya Rais Magufuli kuonyesha kumuunga mkono Makonda, Waziri Nape alifika ofisi za Clouds Media zilizopo Mikocheni saa 3:25 asubuhi, akiwa ameambatana na Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo), Dk Hassan Abbas pamoja na mwenyekiti wa Moat, Reginald Mengi.

Akiwa katika kituo hicho, Nape alisema Serikali inalaani kitendo kilichotokea katika nchi ambayo imesaini mikataba ya kimataifa ya kulinda uhuru wa habari na kwamba sheria zipo na zinapaswa kufuatwa

“Tumeunda timu ya watu watano kufanya kazi kwa saa 24 ili wapate maelezo ya RC baada ya hapo tutaeleza hatua tutakazozichukua kama Serikali. Lakini kabla ya kuchukua hatua zozote, tunataka kusikia kutoka kwa mkuu huyo,” alisema Nape.

Waziri Nape alikifananisha kitendo hicho kama mapinduzi ya kijeshi na kusema anaanza kuona dalili za wanasiasa kukosa ngozi ngumu.

“Kwakweli inatisha, haijawahi kutokea katika historia ya nchi yetu. Hii inatokea tu kwenye nchi zenye mapinduzi ambako wanaopindua huvamia redio na kujitangaza,” alisema Nape.

Alisema huwezi kuzungumzia suala la ulinzi mdogo kuwepo Clouds kwa sababu unaweza ukawepo hata wa polisi, lakini akishakuwepo mkuu wa mkoa hawana cha kufanya.

“Nimeteua kamati ndogo inayoongozwa na mkurugenzi wa habari. Nimewaagiza wamhoji leo (jana) mkuu wa mkoa ili tupate nini kiliwasukuma wafanye walichofanya, halafu kesho (leo) mchana tutakuwa na press conference (mkutano na waandishi) kueleza hatua tutakazochukua,” alisema Nape.

Mengi azungumza

Akizungumzia tukio hilo, mwenyekiti wa Moat alisema wako pamoja na Clouds na watashirikiana kupambana na unyanyasaji kwa vyombo vya habari na kuwataka waandishi kuendelea kufanya kazi bila woga.

Alisema sura moja ya mwandishi wa habari ni kutokuwa mwoga hivyo jambo lililotokea lisiwatie hofu.

“Jambo lililofanyika ni la hatari sana. Na lazima tujiulize mtu huyu (Makonda) anapata wapi ujasiri huu?. Kama alikuja na bunduki hapa anaweza kwenda nazo popote na pengine kuna siku atazitumia,” alisema Mengi.

Alisema ana imani kuwa Rais Magufuli na waziri wa habari wana upendo kwa vyombo vya habari lakini mapenzi hayo lazima yaonyeshwe kwa vitendo.

Kamati ya Bunge yatinga Clouds

Katika hatua nyingine, Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii ilitembelea ofisi za Clouds Media na mwenyekiti wake, Peter Serukamba alisema wametumwa na Spika wa Bunge.

“Alichofanya mkuu wa mkoa kwa namna yoyote ni matumizi mabaya ya madaraka. Sisi kama kamati tunasubiri Serikali wameunda kamati na sisi tutashauri baada ya kupata maoni ya hiyo kamati,” alisema Serukamba.

Huku akisisitiza haja ya waandishi wa habari kulindwa wanapotimiza majukumu yao, Serukamba alisema viongozi wa Serikali hawapaswi kutumia vyombo vya ulinzi na usalama kufanya lolote wanalotaka kinyume cha sheria.

“Leo (jana) amekuja kwenye vyombo vya habari, kesho atakwenda kwenye restaurant, keshokutwa atakwenda kwenye nyumba zetu. Niviombe sana vyombo vya usalama, fanyeni kazi kulingana na sheria zilizowaweka madarakani. Nchi inaendeshwa na sheria,” alisema Serukamba.

Alisema jambo hilo ni gumu kulifikiria na ni dalili za ulevi wa madaraka.

“Nilikuwa najiuliza, wakipanda hapa na mabunduki ingetokea bahati mbaya bunduki ile kukatokea lolote, risasi ikafyatuka akafa mtu, leo tungeongea nini? Huku ndiyo kuchapa kazi?” alihoji.

“Lakini kwa vyovyote vile kilichofanyika hakikubaliki kwa jamii ya Watanzania. Kutoka miaka 50 ya uhuru, hakuna mkuu wa mkoa amewahi kufanya haya. Tumepitisha sheria ile ya habari, lakini na waandishi wa habari walindwe,” alisema.

Hata hivyo, Serukamba aliwataka waandishi na wamiliki wa vyombo vya habari kuepuka kutumiwa na wanasiasa kwa masilahi yao.

“Jambo hili ni fundisho kwa waandishi wa habari. Msikubali kutumiwa na sisi wanasiasa. Inawezekana matokeo ya jambo hili ni kwa sababu sisi wanasiasa tunakuja kwenye vyombo vya habari, tunatengeneza ujamaa na tunaweza kulazimisha mambo ambayo ni nje ya utaratibu,” alisema Serukamba.

Sugu alaani

Akizungumzia tukio hilo, Waziri Kivuli wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Joseph Mbilinyi alisema walioguswa si Clouds Media peke bali tasnia nzima ya habari.

“Kwa kweli kitendo kilichotokea ni cha kulaaniwa. Hii siyo Tanzania tuliyokuwa tukiitarajia na ndiyo maana tuko hapa kunyoosha mambo kama viongozi. Shambulio lililofanywa jana (juzi) si kwa Clouds peke yake, bali ni kwa industry nzima,” alisema Mbilinyi maarufu kwa jina la Sugu.

Mbunge wa Nzega Mjini, Hussein Bashe alimtaka Makonda kuomba radhi kwa jambo alilofanya ili kulinda uadilifu wake.

“Makonda kama kijana anafanya makosa ya kimkakati yanayomharibia sifa kila kukicha. Naamini kiustaarabu si dhambi ukikosea ukaja hadharani kuwaomba radhi Clouds. Ana wajibu wa kuja kuomba radhi kwa kitendo cha kuingia na askari wakiwa na silaha na kutengeneza taharuki hii,” alisema Bashe.

UTPC kuchukua hatua

Nao Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari (UTPC) umeonya kuwa unaweza kumchukulia hatua Makonda, ikiwemo kumtenga katika kazi zake iwapo mamlaka yake ya nidhamu haitamchukulia hatua.

Rais wa UTPC, Deogratias Nsokolo alisema kitendo cha kiongozi wa Serikali kuvamia ofisi akiambatana na askari wenye silaha ni cha jinai na hakijawahi kutokea nchini.

“Mtu yeyote anayetaka kulazimisha habari gani itoke au isitoke anafinya uhuru wa habari kwani kazi ya uandishi wa habari ina miiko yake hiyo na inayotumika kuamua ni habari gani itumie au isitumike,” alisema Nsokolo.

Mkurugenzi wa UTPC, Abubakar Karsan alisema hivi karibuni Serikali imepitisha sheria inayoitwa uhuru wa habari na moja kati ya vipengele katika sheria hiyo inawapa mamlaka Serikali kuchagua habari gani itoke au isitoke, kwa maana hiyo kitendo cha mkuu wa mkoa kuvamia kituo hicho cha habari swali la kujiuliza je, sheria hiyo imeanza kutekelezeka?

TLS watoa kauli

Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Tundu Lissu amemshauri Rais Magufuli atengue uteuzi wa Makonda haraka iwezekanavyo kabla hajachafua zaidi taswira ya Serikali yake.

Pia amemshauri Rais Magufuli kumchukulia hatua stahiki kamanda au mkuu wa kikosi chochote cha jeshi lolote aliyeruhusu askari wake kutumiwa na Makonda kwa namna iliyoripotiwa.

Katika taarifa yake kwa umma, Lissu amesema Makonda hastahili kuendelea kwenye madaraka hayo kwa siku moja zaidi.

Imeandikwa na Ephrahim Bahemu, Elias Msuya, Peter Elias, Ngollo John