Simulizi ya moto ulioua dereva na kuteketeza magari saba

Muktasari:

  • Chrispine Kamugisha akisimulia ajali hiyo alisema ilitokea wakati lori lililokuwa limebeba dizeli likiingia kwenye lango la kituo cha forodha Rusumo kilichopo mpakani mwa Tanzania na Rwanda.

Ngara. Mtu aliyeshuhudia ajali ya moto uliosababisha kifo cha dereva, utingo kujeruhiwa na magari saba kuteketea katika kituo cha forodha Rusumo wilayani Ngara amesimulia jinsi tukio hilo lilivyotingisha eneo hilo.

Chrispine Kamugisha akisimulia ajali hiyo alisema ilitokea wakati lori lililokuwa limebeba dizeli likiingia kwenye lango la kituo cha forodha Rusumo kilichopo mpakani mwa Tanzania na Rwanda.

Kamugisha alisema lori hilo lilionekana kupata hitilafu kwenye mfumo wa breki hivyo lililigonga jingine ndipo moto ulipolipuka na kuunguza mengine yaliyokuwapo eneo hilo.

“Eneo hili lina mteremko mkali kuingia sehemu ya maegesho,” alisema.

Imeelezwa kuwa dereva wa lori lililobeba mafuta alishindwa kutoka na kwamba, utingo alijeruhiwa baada ya kuruka.

Moto huo ambao ulizimwa kwa kutumia helikopta ya Jeshi la Rwanda ulisababisha taharuki eneo la tukio.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Augustino Olomi alimtaja dereva aliyefariki dunia kuwa ni Abdallah Salimu (37) mkazi wa Dar es Salaam na utingo aliyejeruhiwa ni Haji Mohammed (22) pia mkazi wa Dar es Salaam.

Alisema magari ya zimamoto kutoka Karagwe yalifika eneo la tukio na kusaidiana na helikopta ya kijeshi ya Rwanda kuzima moto huo.

“Juhudi zilizofanywa na kikosi cha zimamoto Karagwe na wenzetu kutoka Rwanda kimesaidia kwa haraka kuepusha madhara zaidi,” alisema Kamanda Olomi.

Akizungumzia tukio hilo, Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Michael Mntenjele alisema utingo wa gari lililokuwa limebeba dizeli aliruka na kuumia hivyo alipelekwa katika Hospitali ya Nyamiaga kwa matibabu.

Baada ya moto kuendelea huku kukiwa hakuna magari ya zimamoto, Mntenjele alisema waliwasiliana na viongozi wa Rwanda waliahidi kutuma helikopta iliyofika na kuuzima.

Alisema kukosekana gari la zimamoto wilayani Ngara na hasa kata ya Rusumo ni changamoto katika kuokoa maisha ya wananchi na mali zao.

Wakala wa Forodha Kituo cha Rusumo, Abdul Shakuru alisema gari lililosababisha ajali ni mali ya kampuni ya Lake Oil.

Alisema magari mengine yaliyoteketea ni ya kampuni ya Azam yanayosafirisha mizigo kutoka Tanzania kwenda Rwanda.

Alisema magari yapatayo 60 yaliyokuwapo eneo la kituo. Kwa siku, kituo hicho huhudumia kati ya magari 80 na 100 yanayosafirisha mizigo kwenda Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), huku mengine yakirejea Dar es Salaam.

Shakuru alisema licha ya vituo vya forodha kufanya kazi kwa saa 24 Tanzania na Rwanda, changamoto iliyopo upande wa Ngara ni kutokuwa na maegesho ya uhakika.

Katika kipindi cha miaka mitatu, alisema tukio hilo ni la sita.

Eneo palipotokea ajali ni umbali wa kilomita 40 kutoka Rusumo hadi makao makuu ya Wilaya ya Ngara na kilomita tatu kuingia kituo cha forodha upande wa Rwanda.

Kituo hicho kipo umbali wa kilomita 130 kwenda Karagwe ambako kuna gari la zimamoto.