Sinema ya diwani, majambazi

Muktasari:

  • Alinusurika kuuawa baada ya majambazi hao waliokuwa na bunduki na bastola, kumfyatulia risasi sita alipokuwa akiwafukuza ambazo hata hivyo, hazikumpata.

Moshi. Hii ni kama filamu lakini ndio ukweli, Diwani wa Kata ya Kiborlon Manispaa ya Moshi, Frank Kagoma (Chadema) ameonyesha ujasiri wa hali ya juu alipopambana na majambazi waliokuwa na silaha za moto.

Alinusurika kuuawa baada ya majambazi hao waliokuwa na bunduki na bastola, kumfyatulia risasi sita alipokuwa akiwafukuza ambazo hata hivyo, hazikumpata.

Tukio hilo ambalo lilionekana kama sinema, lilitokea mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya majambazi hayo kuvamia duka la jumla la kuuza mitumba linalomilikiwa na Menti Mbowe na kupora Sh10 milioni.

Katika tukio hilo lililotokea saa tano asubuhi eneo la Kiborlon, majambazi hayo walimjeruhi kichwani mfanyabiashara huyo anayemiliki pia mabasi ya Machame Safaris. Hali ya majeruhi huyo inaendelea vizuri.