Sirro: Tutafungua jalada la uchunguzi ajali ya MV Nyerere

Muktasari:

  • Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Simon Sirro amesema polisi watafungua jalada la uchunguzi kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere

Dar es Salaam. Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Simon Sirro amesema polisi watafungua jalada la uchunguzi kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere.

Kivuko hicho kilizama jana Alhamisi Septemba 20, 2018 katika Ziwa Victoria mita 50 kabla ya kutia nanga Kisiwa cha Ukara.

Kilikuwa kikitokea katika Kisiwa cha Bugolora kuelekea Kisiwa cha Ukara wilayani Ukerewe, kinadaiwa kilikuwa kimepakia zaidi ya abiria 100, wengi wakiwa wanaelekea kwenye gulio.

Sirro aliyepo Kisiwa cha Ukara ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Septemba 21, 2018 katika mkutano wake na waandishi wa habari.

Amesema kinachofanyika kwa sasa ni kuendelea kuokoa miili zaidi na kuwatia moyo waliopoteza ndugu na jamaa, baada ya hapo polisi watachukua hatua zaidi.

“Tuendelee kuwaombea ndugu zetu waliopoteza ndugu na jamaa lakini  tutafungua jalada na kisha tutaanzisha uchunguzi wa tukio hilo na baadaye tutawaambia wananchi nini tumekiona,” amesema.

Endelea kufuatilia MCL Digital kwa taarifa zaidi