TCC yapenya tuzo za mwajiri bora Afrika

Mkurugenzi wa Rasilimaliwatu wa Kampuni ya Sigara (TCC), Angela Mangecha (kulia) na Meneja wa Mafunzo na Maendeleo wa kampuni hiyo, Elia Mshana wakionyesha uthibitisho baada ya TCC kutajwa miongoni mwa waajiri bora barani Afrika na taasisi ya Top Employer katika hafla iliyofanyika jijini Johannesburg, Afrika Kusini juzi. Na Mpigapicha Maalumu

Muktasari:

  • Kufuatia ushindi huo, TCC ambayo ni kampuni tanzu ya Japan Tobacco International (JTI) imesema inadhamiria kufikia kiwango cha juu cha uajiri duniani ili iwe kati ya kampuni zinazopigiwa mfano.

 Kampuni ya Sigara Tanzania (TCC), imetambuliwa kama mmoja wa waajiri bora barani Afrika mwaka 2018 katika hafla iliyofanyika Johanesburg nchini Afrika Kusini.

Kufuatia ushindi huo, TCC ambayo ni kampuni tanzu ya Japan Tobacco International (JTI) imesema inadhamiria kufikia kiwango cha juu cha uajiri duniani ili iwe kati ya kampuni zinazopigiwa mfano.

Mkurugenzi wa rasilimali watu wa TCC aliyepokea tuzo kwa niaba ya kampuni hiyo, Angela Mangecha alisema furaha yao ni kujiunga katika familia ya waajiri bora barani humo.

Miongoni mwa vigezo vinavyotolewa na Taasisi ya Top Employers iliyotoa tuzo ya mwajiri bora barani Afrika, Oktoba 12 ni kwa kampuni kutoa mazingira bora kwa wafanyakazi, kuwalea, kukuza na kuendeleza vipaji katika ngazi za kampuni na kuendelea kuboresha utendaji kazi.

Katika sherehe ya utoaji tunzo hizo kampuni nyingine sita za JTI barani Afrika zilipata tuzo hiyo kwenye nchi zao. JTI yenye makao yake nchini Uswisi imeajiri wafanyakazi 27,000 duniani kote.

Mtendaji mkuu wa Top Employers, David Plink alisema, “Utafiti wetu wa kina umehitimisha kuwa TCC inaunda sehemu ya kikundi cha waajiri wanaoendeleza hali za wafanyakazi wao duniani na watu wao wanathaminiwa vizuri zaidi.”

Mtendaji mkuu wa TCC, Alan Jackson alisema wanajivunia ubora wa watumishi walionao lakini umepatikana kutokana na uwekezaji imara na endelevu ambao wamekuwa wakiufanya.