TLS yajitosa matibabu ya Lissu.

Muktasari:

Taarifa iliyotolewa na Makamu Mwenyekiti wa TLS, Godwin Ngwilimi amesema kiasi hicho wamekipata kutoka kwa watu mbalimbali walijitolea kuchangia wa ndani na nje ya nchi wakiwemo wanachama wa chama hicho.

Dar es Salaam. Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) kimesema kimefanikiwa kukusanya Sh138 milioni kugharamia matibabu ya Rais wa Chama hicho, Tundu Lissu aliyelazwa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Leuven nchini Ubelgiji.

Taarifa iliyotolewa na Makamu Mwenyekiti wa TLS, Godwin Ngwilimi amesema kiasi hicho wamekipata kutoka kwa watu mbalimbali walijitolea kuchangia wa ndani na nje ya nchi wakiwemo wanachama wa chama hicho.

Kuhusu mchanganuo wa fedha hizo, Ngwilimi amesema kimetumika kulipa gharama za matibabu ya Lissu katika Hospitali ya Nairobi, Leuven na visa kwa watu watatu wakiwa nchini Ubelgiji.

Ngwilimi ametoa shukuran kwa wale wote waliojitokeza kuchangia matibabu ya Lissu ambaye pia ni mbunge wa Singida Mashariki na mwanasheria mkuu wa Chadema.

Lissu aliyeshambuliwa kwa risasi zaidi ya 30 na watu wasiojulikana Septemba 7, 2017 akiwa katika makazi yake mjini Dodoma ambapo alipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Dodoma na usiku wa siku hiyo alihamishiwa Hospitali ya Nairobi alikolazwa hadi Januari 6 baada ya kahamishiwa Leaven, Ubelgiji kwa mazoezi ya viungo na saikolojia.