TRA yawaonya wafanyabiashara

Muktasari:

Kichere imewaomba wananchi kutoa taarifa kwa TRA juu ya mfanyabiashara au kampuni yoyote inayojihusisha na vitendo vya magendo na ukwepaji kodi.


Dar es Salaam. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imewaonya wafanyabiashara wanaojihusisha na   magendo, ukwepaji kodi kupitia viwanja vya ndege, vituo vya forodha mipakani, njia za panya na bandari bubu kuacha mara moja.

Taarifa iliyotolewa leo Februari 18, 2018 na mamlaka hiyo imesema Kamishna Mkuu wa TRA, Charles Kichere amesema hatua kali za kisheria zitaendelea kuchukuliwa kwa mfanyabiashara yeyote atakayebainika kusafirisha bidhaa kwa kutumia njia za magendo na kukwepa kodi.

Imesema miongoni mwa hatua hizo ni kutaifishwa mali zote zitakazokamatwa na chombo kilichotumika kusafirisha au nyumba iliyohifadhi bidhaa hizo.

Taarifa hiyo imesema kukwepa kodi ni kosa la jinai kwa mujibu wa sheria ya forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2005 na sheria  ya usimamizi wa kodi ya mwaka 2015. 

Imesisitiza kuwa ukwepaji kodi husababisha mambo mengi, ikiwamo kuikosesha Serikali mapato halali ya kuimarisha uchumi ambayo yangeiwezesha kutoa huduma za jamii kwa wananchi.

Kichere imewaomba wananchi kutoa taarifa kwa TRA juu ya mfanyabiashara au kampuni yoyote inayojihusisha na vitendo vya magendo na ukwepaji kodi.

Hivi karibuni, TRA ilikamata na kutaifisha bidhaa mbalimbali zikiwamo tani moja ya sukari na chumvi, majani ya chai mifuko 18, mirungi kilo16, vifaranga vya kuku 5,000 na mayai kasha 416 katika mpaka wa Namanga mkoani Arusha zikitokea Kenya kupitia njia zisizo rasmi.