TRL yahamisha kituo kwa muda

Muktasari:

TRL yaeleza sababu za kuhamisha kituo na mikakati ya kukarabati miundombinu ya reli iliyoharibika kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.

Dar es Salaam. Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) imehamishia kwa muda huduma za usafiri wa treni ya kwenda bara katika kituo cha Morogoro kuanzia leo (Jumamosi) badala ya Dar es Salaam kama ilivyokuwa hapo awali.

Kaimu Kamishna wa Idara ya Masoko, Shaban Kiko amesema kuwa mabadiliko hayo yamekuja baada ya miundombinu kuharibika kwenye  kipande cha reli kati ya Dar es Salaam na Ruvu na daraja kutitia upande mmoja. 

Kiko amesema abiria wote ambao walitakiwa kusafiri leo (Ijumaa) wanatakiwa wafike kituo kikuu cha reli kesho (Jumamosi) kabla ya saa moja asubuhi, ambapo watasafirishwa kwa mabasi hadi Morogoro.

Amesema mamlaka husika zinaendelea na ukarabati wa daraja hilo ili njia hiyo ya reli ianze kutumika mapema iwezekanavyo.

“Tayari Mwenyekiti wa Bodi ya TRL, Profesa John Kondoro na wajumbe wengine asubuhi ya leo wametembelea  eneo la daraja kufanya tathmini ili bodi itoe maelekezo yake kuhusu maandalizi ya kazi za ukarabati wa daraja hilo,”amesema.