TTCL yaipa Serikali gawio la Sh1.5bilioni

Muktasari:

Shirika hilo lilipata faida ya Sh29.2 bilioni kabla ya kukatwa kodi.

Dar es Salaam. Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), limetoa gawio la Sh1.5bilioni kwa Serikali, fedha zilizotokana na faida ya Sh28.5 bilioni ya shirika hilo kwa mwaka jana.

 

Shirika hilo lilipata faida ya Sh29.2 bilioni kabla ya kukatwa kodi.

 

Akizungumza leo Juni 21 mbele ya Rais John Magufuli wakati wa hafla ya kupokea gawio hilo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Waziri Kindamba amesema faida hiyo inatokana na mabadiliko makubwa yaliyoanza kuonekana kupitia uongozi wa awamu ya tano.

 

“Tuliahidi kutoa gawio la Sh1 bilioni, lakini baada ya bodi ya shirika kukaa ikaamua kuongeza gawio hilo baada biashara kwenda vizuri,”amesema.

 

Kindamba amesema katika juhudi za kuimarisha shirika hilo, wameanza kutekeleza maagizo ya Serikali baada ya kupunguza safari za nje kwa waendaji wake na kufuta mikataba mibovu isiyokuwa na manufaa kwa shirika hilo.

 

Hafla hiyo imehudhuriwa na Mwenyekiti wa Bodi ya TTTCL, Omar Nundu huku Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akishiriki kwa njia ya teknolojia ya mawasiliano ya video moja kwa moja kutoka Dodoma.