Telack amwapisha Macha, ampa neno

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkulru wakati alipowasili kwenye viwanja vya ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kahama  kuzungumza na watumishi wa Umma, mkoani Shinyanga. Mkuu huyo wa wilaya alitenguliwa wadhifa huo na Rais John Magufuli muda mchache baada ya tukio hilo. Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu 

Muktasari:

Uteuzi wa Macha ulifanyika Jumapili mchana baada ya Rais Magufuli kutengua uteuzi wa aliyekuwa mkuu wa wilaya hiyo Fadhili Nkurlu.

Kahama. Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Zainab Telack amemwapisha Mkuu wa Wilaya ya Kahama Anamlingi Macha kisha kumtahadharisha kuwa wilaya hiyo siyo ya kuingia kizembe bali inahitaji mikakati.

“Kahama kuna changamoto nyingi ambazo ili ufanikiwe lazima uwe kamanda aliekamilika,” amemueleza Telack.

Pia  amemshauri kuwa na  ushirikiano na viongozi wenzake bila kuwa na uamuzi wa pekee na  aitumie vizuri kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya.

Baada ya kuapishwa katika makao makuu ya wilaya hiyo leo Julai 17, pia Telack alimtaka Macha kuhakikisha anatekeleza maagizo ya Rais John Magufuli kuwapelekea maendeleo wananchi wa wilaya hiyo.

Naye Mwenyekiti wa  CCM wilaya hiyo, Thomas Muyomba amemtaka Macha kusimamia vizuri utekelezaji wa ilani ya CCM na kuahidi kumpatia ushirikiano kila patakaohitajika kufanya hivyo.

 “Wananchi wa Kahama ni wasikivu hivyo wana imani nawe kama ulivyoaminiwa na Rais Magufuli kuja kufanya kazi hapa,” amesema

Hata hivyo, Macha hakuweza kusema lolote na atazungumza wakati mwingine pindi  atakapopata muda mwingine wa kuzungumza na kutoa mikakati yake.

Uteuzi wa Macha ulifanyika Jumapili mchana baada ya Rais Magufuli kutengua uteuzi wa aliyekuwa mkuu wa wilaya hiyo Fadhili Nkurlu wakati akiwa kwenye ziara ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye jana alimaliza ziara yake ya siku nne wilayani hapo.