Tembo wavamia makazi

Muktasari:

  • Wananchi watakiwa kuwa watulivu na wasiwachokoze wala kuwashambulia tembo hao

Same. Wakazi wa kata nne za Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro, wameeleza kuishi kwa hofu baada ya tembo wanaodaiwa kutoka hifadhi za Kenya, kuvamia maeneo yao na kutishia.

Tembo hao wameingia kwa makundi makubwa wakidaiwa kutokea Hifadhi ya Taifa ya Tsavo, Kenya na kuvamia kwenye makazi na mashamba usiku.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wakazi wa maeneo hayo wamesema miaka ya nyuma, tembo walikuwa wakiingia kwenye mashamba na kuharibu mashamba lakini sasa wanaingia hadi kwenye makazi ya watu.

Mmoja wa wakazi hao walioathirika na kadhia hiyo, John Msuya amezitaka mamlaka za Serikali zinazohusika na usimamizi na udhibiti wa wanyamapori kuchukua hatua kabla hawajaleta madhara.

Mkazi wa Kitongoji cha Kandoto, Kata ya Kisima, Loveness Cheavo amesema ana siku ya nne yeye na familia yake wamehama katika makazi yao na kuhamia kwa ndugu wakiwahofia tembo hao.

Mkuu wa Wilaya ya Same, Rosemary Senyamule amewataka wananchi kuwa watulivu na wasiwachokoze wala kuwashambulia tembo hao kwa kuwa wanaweza kuleta madhara zaidi ya kiusalama.

Amesema kwa kushirikiana na Halmashauri ya Same na Idara ya Misitu na Wanyamapori, wanajitahidi kuwadhibiti na tayari wametoa taarifa kitengo maalumu cha udhibiti jijini Arusha.