Thamani ya shilingi yahojiwa bungeni

Muktasari:

Amesema licha ya kuwepo kwa matamko mengi lakini bado maeneo mengi Watanzania wanalazimishwa kutumia dola badala ya shilingi ya Tanzania.

Mbunge wa Viti Maalumu Chadema, Devotha Minja ameitaka Serikali kutoa majibu ina mpango gani kuchukua hatua ili kulinda thamani ya shilingi kama nchi nyingine zinavyolinda fedha zao.

Mbunge huyo amesema licha ya kuwepo kwa matamko mengi lakini bado maeneo mengi Watanzania wanalazimishwa kutumia dola badala ya shilingi ya Tanzania.

Akijibu swali hilo bungeni leo Jumatatu, Aprili 16, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Ashatu Kijaji amesema matumizi ya fedha za kigeni sambamba na shilingi ya Tanzania yanasimamiwa na Sheria ya Matumizi kwa Fedha za Kigeni ya 1992.

Dk Kijaji amesema Desemba 2017 waziri wa fedha alitoa tamko kwa umma kuwa ifikapo Januari Mosi, 2018, matumizi ya fedha za kigeni yazingatie mambo halisi yaliyopo na ikiwemo bei zote kutangazwa kwa shilingi ya Tanzania.

Kuhusu utitiri wa maduka ya kubadilisha fedha,  amesema hadi sasa Serikali imeshafungia jumla ya maduka 92 na itaendelea kufungia kwa watakaokiuka sheria ili kulinda shilingi ya Tanzania.

"Mkazi yeyote wa Tanzania asilazimishwe kulipia bidhaa au huduma yoyote hapa nchini kwa fedha za kigeni na vyombo vya dola viwachukukie hatua za kisheria wale wote watakaobainika kukiuka maagizo ya Serikali," amesema Kijaji