Trump, Putin uso kwa uso leo

Muktasari:

> Marekani na Urusi zimekuwa na uhasama ulioibuka wakati wa Rais Barack Obama hivyo inatarajiwa kwamba kukutana kwa Trump na Putin kunaweza kuwa mwanzo wa kumaliza uhasama wa mataifa hayo mawili.

Marekani. Rais wa Marekani, Donald Trump na mwenzake wa Urusi ,Vladmir Putin wanatarajiwa kukutana ana kwa ana katika mkutano wa mataifa yaliyo na uwezo mkubwa duniani ya G20 katika mji wa Hamburg nchini Ujerumani leo Ijumaa, Julai 7.

Wawili hao wamesema kwamba wanataka kuimarisha uhusiano wao ambao uliharibika wakati wa mgogoro wa Syria na Ukraine mbali na madai ya Urusi kuingilia kati uchaguzi wa Marekani.

Kabla ya mkutano huo, maafisa wa polisi 76 walijeruhiwa  wakati wakikabiliana na waandamanaji .

Viongozi hao wawili wanatarajiwa kukutana Ijumaa mchana  baada ya mkutano wa G20.

Vyombo vya habari nchini Urusi vimesema kuwa mkutano huo utakuwa wa saa moja, lakini baadaye ripoti zinasema kuwa huenda ukachukua dakika 30.

Marais hao wanatarajiwa kujadiliana zaidi kuhusu maswala ya Syria na Ukraine.

Siku ya Alhamisi, Trump alitumia hotuba yake nchini Poland kutoa wito kwa Urusi kuacha kuyumbisha Ukraine na mataifa mengine.

''Moscow pia ni lazima isitishe usaidizi kwa serikali mbaya kama vile Syria na Iran na kujiunga na jamii ya mataifa yanayowajibika,'' amesemaTrump.