UVCCM yaanzisha vita wasiotekeleza ahadi

Katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Wilaya ya Ileje, John Mwakifuna (kushoto) akitoa maelezo ya utekelezaji wa Ilani ya chama hicho kwa Mwenyekiti wa umoja huo kwa mikoa ya Mbeya na Songwe, Amani Kajuna (katikati) alipofanya ziara mwishoni mwa wiki kukagua miradi ya maendeleo wilayani humo. Picha na Hawa Mathias

Muktasari:

Mwakifuna alisema hayo mwishoni mwa wiki kwenye kikao na Mwenyekiti wa UVCCM wa mikoa ya Songwe na Mbeya, Aman Kajuna aliyetembelea wilayani hapa kukagua miradi ya vijana.

Ileje. Katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) wilayani hapa, John Mwakifuna amesema chama hicho kinakabiliwa na changamoto nyingi kutokana na baadhi ya viongozi wake kutotekeleza ahadi zao kwa wananchi.

Mwakifuna alisema hayo mwishoni mwa wiki kwenye kikao na Mwenyekiti wa UVCCM wa mikoa ya Songwe na Mbeya, Aman Kajuna aliyetembelea wilayani hapa kukagua miradi ya vijana.

“Tunapata wakati mgumu kwa wapiga kura na kuhojiwa maswali magumu kutokana na wagombea   waliopita katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kutotekeleza ahadi na hasa zinazohusu kuboresha miundombinu ya barabara, zahanati kila kijiji na pembejeo za kilimo kutofika kwa wakati,” alisema.

Alisema baadhi ya wenyeviti wa vijiji, madiwani na wabunge hawawatembelei wananchi kujua kero zao na kuzitafutia majawabu.