UVCCM yapata viongozi wapya

Mwenyekiti Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Kheri James

Muktasari:

James ameibuka mshindi kwa kupata kura 319 kati ya kura 583 zilizopigwa.

Dar es Salaam. Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) umemchagua Kheri James kuwa mwenyekiti wake kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.

James amepata kura 319 kati ya kura 583 zilizopigwa akimwacha kwa mbali mpinzani wake, Thobias Mwesiga aliyepata kura 127.

Uchaguzi huo uliofanyika jana Jumapili Desemba 10,2017 ukihusisha wagombea saba kwa nafasi ya mwenyekiti.

Katika uchaguzi wa makamu mwenyekiti wa UVCCM, Thabia Mwita ameshinda kwa kupata kura 286 dhidi ya mpinzani wake Rashid Mohamed Rashid aliyepata kura 282.

Msimamizi wa uchaguzi huo alikuwa William Lukuvi ambaye pia ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Wagombea wengine waliochaguliwa ni mwakilishi wa vijana katika jumuiya ya Umoja wa Wanawake (UWT), Dotto Nyirenda; mwakilishi wa vijana kwenda Jumuiya ya Wazazi, Amir Mkalipa na wawakilishi watatu wa Tanzania Bara kwenda Baraza Kuu la UVCCM ambao ni Rose Manumba, John Katarahiya na Secky Kasuga.

Wengine ni wawakilishi wawili wa Zanzibar kwenda Baraza Kuu la UVCCM ambao ni Nasra Haji na Abdallah Rajabu.

Pia, wajumbe wawili kutoka Zanzibar wanaokwenda Halmashauri Kuu ya Taifa, Abdallaghari Idrisa Juma na Maryam Mohamed Khamis.

Wengine waliochaguliwa ni wajumbe watatu kutoka Tanzania Bara wanaokwenda Halmashauri Kuu ambao ni Sophia Kizigo, Mussa Mwakitinya na Keisha.

Akizungumza baada ya kutangazwa mshindi, mwenyekiti James amewataka vijana kufanya kazi kwa bidii na kutekeleza maagizo yaliyotolewa na mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli.

Ameagiza viongozi wa umoja huo hotuba ya Rais Magufuli aliyoitoa jana akifungua mkutano wa tisa wa UVCCM ichapishwe na nakala zisambazwe kwa vijana mikoani na wilayani ili kutekeleza maagizo aliyoyatoa ikiwamo kupambana na rushwa na ubadhirifu wa mali za jumuiya hiyo.