Ubunifu wa kuvutia wa wanafunzi shule ya kata

Muktasari:

Katika ulimwengu huu wa sayansi na teknolojia, ubunifu unaweza kumsaidia katika soko la ajira pindi anapohitimu.

Kwa kawaida, mwanafunzi anayejitambua hategemei anachofundishwa na mwalimu pekee, bali kujiongeza kwa kuwa mbunifu.

Katika ulimwengu huu wa sayansi na teknolojia, ubunifu unaweza kumsaidia katika soko la ajira pindi anapohitimu.

Wanafunzi Naimah Mohammed na Stephano Chacha kutoka Shule ya Sekondari Vingunguti, wameamua kuishi kwenye uhalisia huu.

Pamoja na umri wao mdogo, vichwa vyao vinachemka baada ya kubuni mashine ya kupalilia inayotumia nishati ya jua.

Ubunifu wao unaweza kutajwa kama kielelezo cha umuhimu wa shule za kata zilizosambaa kila kona ya nchi. Wamewatoa kimasomaso wanafunzi wenzao, hasa dhidi ya baadhi ya watu wanaozitazama shule za kata kwa jicho la pembeni.

Wanafunzi hawa wenye ndoto ya kuja kuwa wahandisi baadaye, walitengeneza mashine hiyo Mei mwaka huu kwa lengo la kuwarahisishia wakulima na kutatua changamoto za kilimo zinazowakabili wakulima nchini.

“Kabla ya hapo tulifikiria kitu gani tutengeneze, tukakubaliana kubuni kitu ambacho kama kitaungwa mkono kitakuwa na manufaa katika jamii,”anasema Naimah.

Baada ya kubaini kuwa changamoto inayowakabili wakulima wengi nchini, ni kulima kilimo cha kizamani hasa kutumia jembe la mkono, fikra ikawa ni kutengeneza mashine rahisi ya kupalilia.

Kifaa hicho kimetengenezwa kwa vifaa vitano ambavyo ni paneli ya nguvu ya jua, swichi, mota na betri. Kinatumia jembe lenye meno mithili ya msumeno sehemu ya kulimia.

“Hili jembe lina mfumo wa kifaa ambacho kinabebwa mgongoni kama begi. Kifaa hiki kinabeba vifaa vyote vinavyotumia nishati ya jua, sehemu ya pili ni jembe,’’ anasema na kuongeza;

‘Ni jembe la kawaida lakini lina meno sehemu ya kulimia na mpini wake kwa juu tunaweka swichi ambayo ikibonyezwa jembe linapalilia; kazi ya mkulima ni kushikilia tu.’’

Wanasema mashine hiyo ina uwezo wa kupalilia eneo la ekari moja kwa siku mbili au tatu. Aidha. inaweza kutumika kujaza udongo kwenye mashina ya mazao kama vile karanga.

Naimah ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule hiyo iliyopo Vingunguti jijini Dar es Salaam,anasema jembe la mkono lina athari kwa wakulima, hivyo wanapaswa kubadilika na kuanza kutumia vifaa vya kisasa.

“Mkulima anapotumia jembe la kawaida itamlazimu kuinama, katika hali ya kawaida mtu anapoinama kwa muda mrefu lazima atapata maumivu ya mgongo, hivyo hata uzalishaji unapungua kwa kuwa atatumia muda mrefu kupalilia shamba” anasema.

Kubuni mashine hiyo siyo mwisho wa safari yao, kwani wanasema wanatarajia kubuni kitu kingine kikubwa ikiwa watawezeshwa.

Chacha anasema baada ya ubunifu wao huo kushinda katika mashindano ya wanasayansi bora chipukizi yaliyofanyika Agosti mwaka huu, huo ni mwanzo mzuri wa kutangaza kifaa chao.

Wito kwa Serikali

Chacha anatoa rai kwa Serikali kuwaunga mkono kwa kuufanyia kazi ubunifu wao na hata kuwawezesha kifedha.

“ Jembe hili linaweza kumsaidia mkulima moja kwa moja, kwa hiyo ubunifu unaongeza maendeleo ya nchi,”anaeleza.

Anasema kupitia jembe hilo ambalo ni rahisi kutumia na lisilotumia gharama yoyote zaidi ya nishati ya jua, wananchi wataongeza kipato kwa kulima mazao mengi, na jamii nzima itanufaika.

“Mashine hii tuliyoigundua ni mbadala wa kutumia jembe la mkono, nchi za wenzetu wanatumia hizi teknolojia kwa ajili ya kilimo, hivyo hata sisi mashine hii kama itapewa kipaumbele inaweza kuwa suluhisho katika sekta ya kilimo,” anasema.

Benitho Sutta ni mwalimu wa somo la Fizikia shuleni hapo. Anasema baada ya kupokea wazo kutoka kwa Naomi na Chacha, aliahidi kutoa ushirikiano ili kufanikisha wazo lao la kutengeneza kifaa cha kipekee nchini.

Anasema wazo lao ni la kipekee kwani limejikita kutatua changamoto katika sekta ya kilimo nchini.

“Wanafunzi wengi wanakimbilia masomo ya sanaa na hicho ndicho kinachowakwamisha wengi kwa kigezo kuwa masomo hayo ni mepesi, lakini ukweli ni kwamba masomo ya sayansi yanaweza kumweka mwanafunzi katika nafasi nzuri ya kujiajiri kupitia ubunifu,” anasema.

“Nimegundua kuwa wanafunzi wengi ni wabunifu; wana mawazo mengi kichwani lakini yanakuwa kama michezo ya kuigiza kwa sababu namna ya kuyaleta katika hali halisi inakuwa ngumu kuyatekeleza,”anasema na kuongeza:

“Mfano jembe hili limegharimu kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya kununua vifaa mbalimbali na kupeleka kwa fundi kuchomelea, kwa hiyo kiasi kikubwa cha fedha kimetumika.

Chacha na Naimah wanalia kutotembelewa na kiongozi yeyote wa kuwapa moyo au kuwasaidia kuhusu ubunfu wao.

Mwalimu wao anasema kama wangepata msaada wangefanya vizuri zaidi katika ubunifu na kutengeneza mashine nyingi zinazoweza kutumika nchi nzima.