Ukuta wa Chadema marufuku Kilimanjaro

Moshi.Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Said Meck Sadick amesema kutokana na maelekezo yanayoendelea kutolewa na viongozi wa Chadema ambayo yanaelekeza kufanya maandamano nchi nzima anapiga marufuku operesheni ya Ukuta kufanyika mkoani hapa.

Akizungumza ofisini kwake leo Sadick alisema kuwa kikako cha kamati ya ulinzi mkoani hapa kilichofanyika jana kimeazimia kuwatahadharisha wananchi hususani vijana ambao wamekuwa wakishawishika kirahisi kufanya maandamano yasiyokuwa na tija.

“Serikali ya mkoani hapa inatoa onyo kwa viongozi wanaoendelea kuratibu na kufanya mikutano ya usiku inayolenga kujadili namna ya kufanikisha mpango wao ambao ni haramu waache mara moja kwakuwa tutawatia nguvuni,”alisema.

Alisema kuwa taarifa na majina ya viongozi hao wanayo na wameyahifadhi hivyo aliwataka waache uchochezi na uhamasishaji wa mikutano isiyokuwa na manufaa ambapo ni kinyume na sheria.